Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 26 Works, Transport and Communication Ofisi ya Rais TAMISEMI. 210 2016-05-23

Name

Sophia Hebron Mwakagenda

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA aliuliza:-
Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe ni sehemu ya ghala la chakula la Taifa katika mikoa mitano (5) inayolima chakula kwa wingi nchini Tanzania; lakini kikwazo kikubwa ni usafirishaji wa mazao kufikia masoko ya nje ya Wilaya; Halmashauri imeomba ongezeko la bajeti ya barabara kufikia shilingi bilioni 7,969,000 ili kuweza kukarabati barabara zote muhimu na kuwezesha wakulima kusafirisha mazao yao kwa urahisi na hatimaye kuongeza kipato cha Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe:-
Je, Serikali ipo tayari kukubali ombi la Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe la kuongeza fedha katika bajeti ya 2016/2017?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sophia Hebron Mwakagenda, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe iliandaa makisio ya bajeti ya shilingi bilioni 7.9 kwa ajili ya matengenezo ya barabara katika bajeti ya mwaka 2016/2017. Hata hivyo, kutokana na ukomo wa bajeti, fedha zilizoidhinishwa ni shilingi milioni 920 ambazo zitatumika kwa ajili ya matengenezo ya barabara na ujenzi wa madaraja. Katika mwaka wa fedha 2015/2016, Halmashauri hiyo ilitengewa shilingi milioni 870 na tayari Serikali imepeleka shilingi milioni 157.9.
Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha za Mfuko wa Barabara katika bajeti ya mwaka 2016/2017 ni shilingi bilioni 247.5 ambazo endapo zingegawanywa sawa kwa kila Halmashauri zote 181 zilizopo, kila Halmashauri ingeweza kupata bajeti ya shilingi bilioni 1.3 tu. Hivyo, mara zote mahitaji yamekuwa ni makubwa kuliko uwezo wa rasilimali fedha kukidhi mahitaji hayo, ndiyo maana tunaweka vipaumbele ili kutekeleza mambo machache kwanza kulingana na uwezo uliopo kibajeti. Serikali itaendelea kuongeza bajeti kwa ajili ya barabara kadri uwezo utakavyowezekana.