Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 27 Health and Social Welfare Ofisi ya Rais TAMISEMI. 221 2016-05-24

Name

Atupele Fredy Mwakibete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busokelo

Primary Question

MHE. FREDY A. MWAKIBETE aliuliza:-
Serikali imekuwa ikiahidi kusogeza huduma za afya karibu na wananchi na kuna umuhimu mkubwa wa kuwa na Zahanati kwa kila Kijiji na Kituo cha Afya kila Kata na Hospitali kwa kila Wilaya ili kuwaondolea kero wananchi wanaosafiri umbali mrefu kufuata huduma za afya na wengine kupoteza maisha wakiwa njiani:-
Je, ni lini Serikali itatekeleza mpango huo wa kuwa na Zahanati kwa kila Kijiji, Kituo cha Afya kwa kila Kata na Hospitali kwa kila Wilaya?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Fredy Atupele Mwakibete, Mbunge wa Busokelo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa Zahanati kwa kila kijiji, Vituo vya Afya kila Kata na Hospitali kila Wilaya, unafanyika kwa ushirikiano kati ya wananchi na Halmashauri kupitia Mpango wa Fursa na Vikwazo kwa Maendeleo (O&OD).
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu kubwa ya miradi hii huibuliwa na kutekelezwa na wananchi wenyewe na Halmashauri huchangia nguvu kidogo ili kukamilisha miradi hiyo. Serikali kwa kushirikisha nguvu za wananchi, inaendelea na ujenzi wa Zahanati, Vituo vya Afya na Hospitali kila Wilaya. Ujenzi huo unafanyika chini ya Mpango wa Maendeleo ya Afya ya Msingi yaani MMAM, ambapo vituo vya kutolea huduma za afya vimeongezeka kwa mwaka 2016 hadi 6,935 katika mwaka 2014/2015 sawa na ongezeko la asilimia 31.9. Aidha, utekelezaji wa program hii unaendelea, ambapo katika mwaka 2016/2017 Halmashauri zimetengewa shilingi bilioni 182.5 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya afya.
Mheshimiwa Naibu Spika, kipaumbele kimetolewa katika kukamilisha miradi viporo, badala ya kuanzisha miradi mipya. Ofisi ya Rais TAMISEMI, inafanya tathmini ya utekelezaji wa MMAM ili kujua idadi ya vijiji ambavyo havina Zahanati. Kata ambazo hazina Vituo vya Afya na Wilaya ambazo hazina Hospitali. Lengo la tathmini hiyo ni kuhakikisha maeneo haya yanapewa kipaumbele na kutengewa bajeti ili kuongeza huduma za afya karibu na wananchi.