Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 4 Sitting 1 Justice and Constitutional Affairs Wizara ya Katiba na Sheria 13 2016-09-06

Name

Issa Ali Abbas Mangungu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbagala

Primary Question

MHE. ISSA A. MANGUNGU aliuliza:-
Jimbo la Mbagala lina wakazi zaidi ya 800,000 kutokana na sensa ya watu na makazi lakini ina Mahakama ya Mwanzo Kizuiani tu.
(a) Je, kwa nini Serikali imeshindwa kujenga mahakama katika Jimbo la Mbagala kwa kuzingatia idadi kubwa ya wakazi?
(b) Kwa kuwa kuna mahitaji makubwa ya huduma za mahakama Jimbo la Mbagala katika Kata za Chamazi, Mbande, Kijichi, Kibungwa, Kibondemaji na Tuangoma; je, Serikali ipo tayari kujenga mahakama katika kata hizo hata kwa mpango wa dharura?

Name

Dr. Harrison George Mwakyembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyela

Answer

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, namshukuru Mungu kukuona na afya njema.
Napenda kujibu swali la Mheshimiwa Issa Ali Mangungu, Mbunge wa Mbagala, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa kifungu cha 4 cha Sheria ya Mahakimu Namba 2 ya mwaka 1984, Mahakama ya Wilaya huanzishwa kwa kuzingatia kuwepo kwa Mamlaka ya Wilaya ya Kiserikali. Uanzishwaji wa Makahama ya Wilaya hutegemeana na hali ya upatikanaji wa rasilimali watu, rasilimali fedha na miundombinu mingine kama majengo, viwanja na kadhalika.
Mheshimiwa Spika, aidha, uanzishwaji wa Mahakama za Mwanzo (Primary Courts) huhitaji walau kila kata za Wilaya husika iwe na Mahakama ya Mwanzo moja ingawa hakuna kizuizi kwa mamlaka kuanzisha Mahakama za Mwanzo zaidi ya moja kwenye kata moja kutegemeana na mahitaji ya eneo husika na vipaumbele vya mahakama na wananchi.
Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Dar es Salaam kwa sasa una Wilaya tano kiutawala (Ilala, Temeke, Kinondoni, Kigamboni na Ubungo) na kata zaidi ya 102 zenye idadi ya wakazi zaidi ya 5,000,000 wanaohitaji huduma hii muhimu, ni dhahiri kwa takwimu tajwa hapo juu Mkoa wetu wa Dar es Salaam unahitaji Mahakama za kisasa za Wilaya tano na Mahakama za Mwanzo 102 angalau kukidhi kila kata ukilinganisha na mahakama 12 zilizopo sasa hivi.
Mheshimiwa Spika, kwa kutambua mahitaji hayo, tayari Wizara kwa kushirikiana na mahakama tumepeleka maombi maalum kwa uongozi wa Mkoa wa Dar es Salaam, Wilaya na Halmashauri zake waweze kutupatia viwanja vya umma (public plots) vyenye kutosheleza mahitaji ya Mahakama za Mwanzo na Wilaya kwenye maeneo ya makazi ya mjini na yenye shughuli nyingi kama Jimbo la Mbagala. Tunashukuru uongozi wa baadhi ya Wilaya kwa kuanza kutupatia viwanja ambavyo tumeanza kufanya maandalizi ya ujenzi wa mahakama hizo.
(b) Mheshimiwa Spika, tunamuhimiza Mheshimiwa Mbunge na uongozi wa Mkoa wa Dar es Salaam pamoja na Wilaya zake kutoa viwanja vyenye nyaraka rasmi ili tuweke kwenye mpango wa dharura wa ujenzi wa Mahakama za Mwanzo kwenye maeneo yenye kuhitaji kama vile Chamazi, Mbande, Kijichi, Kiburugwa na Kibondemaji.