Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 11 Sitting 27 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 360 2023-05-17

Name

Dorothy George Kilave

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Temeke

Primary Question

MHE. JANEJELLY J. NTATE K.n.y. MHE. DOROTHY G. KILAVE aliuliza: -

Je, nini tamko la Serikali kuhusu Kitambulisho cha Taifa kuwekwa ukomo wa kutumika?

Name

Sagini Jumanne Abdallah

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Butiama

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dorothy George Kilave, Mbunge wa Jimbo la Temeke, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Vitambulisho vya Taifa vilivyotolewa hadi mwaka 2022 vilikuwa na tarehe ya ukomo wa kutumika. Serikali imefanya marekebisho ya Kanuni za Usajili na Utambuzi wa Watu za mwaka 2014 ikiwemo Kanuni ya 7(3)(a) ambayo inaainisha taarifa zilizopo katika uso wa Kitambulisho cha Taifa zinazohusiana na tarehe ya ukomo wa muda wa matumizi ya Kitambulisho cha Taifa. Ili kuondoa ukomo wa matumizi, marekebisho hayo yalitangazwa rasmi katika Tangazo la Serikali (GN) Na. 96 la tarehe 17 Februari, 2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ina maana kwamba, Vitambulisho vya Taifa kwa raia ili kuwezesha Vitambulisho vinavyofikia ukomo wake baada ya kipindi cha miaka kumi vitaendelea kutumika baada ya muda huo. Napenda kufafanua zaidi kwamba Namba za Utambulisho (NIN) zilizopo katika vitambulisho hivyo, hazina ukomo wa muda wa matumizi. Aidha, marekebisho hayo hayatahusu muda wa matumizi ya Vitambulisho vya Taifa kwa Wageni Wakaazi (Legal Residents) na Wakimbizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa wito kwa watoa huduma wanaotumia vitambulisho vya Taifa kuwatambua wateja wao, kuendelea kutambua vitambulisho vyenye tarehe za ukomo, nakushukuru.