Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 48 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 417 2016-06-22

Name

Anatropia Lwehikila Theonest

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SOPHIA M. SIMBA (K.n.y. MHE. ANATROPIA L. THEONEST) aliuliza:-
Kuna mgogoro wa ardhi baina ya wananchi wa Kipunguni „A‟ na Kipunguni Mashariki dhidi ya Mamlaka ya Uwanja wa Ndege Jijini Dar es Salaam. Wananchi hao wanapinga uthamini uliofanywa na fidia kidogo kwa kikundi cha watu wachache, huku wengine wakizuiwa kuendeleza maeneo yao?
(a) Je, ni lini Serikali itaenda kumaliza mgogoro huo uliodumu tangu 2007?
(b) Je, Serikali ipo tayari kuwapa fidia ya kiwango cha soko wananchi waliozuiwa kuendeleza maeneo yao na kuendelea kubaki maskini kwa muda wote huo?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali Na. 417 la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la Kipunguni “A” na Kipunguni Mashariki pamoja na maeneo ya Kipawa pamoja na Kigilagila ni maeneo yaliyotwaliwa na Serikali kupitia Mamlaka ya Viwanja vya Ndege mwaka 1997. Uthamini wa maeneo haya ulifanywa na Kampuni ya Tanvaluers and Property Development ambayo ni kampuni binafsi ya uthamini na ilifanya mwaka 1997. Hata hivyo, malipo ya fidia hayakuweza kufanyika kwa wakati. Mwaka 2011 Serikali iliamua kuanza kuwalipa wananchi hao fidia kwa kuanza na eneo la Kipawa na Kigilagila.
Mheshimiwa Naibu Spika, ikumbukwe kuwa Sheria iliyotumika kufanya uthamini huo ilikuwa ni ile ya Utwaaji Ardhi ya mwaka 1967 yaani (The Land Acquisition Act of 1967) ambayo ilipwaji wa fidia ulipaswa kuzingatia yafuatayo:-
(i) Maendelezo pekee (yaani majengo na mazao katika eneo);
(ii) Kiwanja mbadala; na
(iii) Riba ya 6% kwa kila mwaka pindi malipo yanapocheleweshwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka 2010 wananchi hao walifungua kesi Mahakama Kuu wakipinga kulipwa fidia kwa kutumia sheria ya zamani, wananchi walishindwa kesi hiyo, kwani mchakato wa utwaaji wa eneo hilo ulianza ndani ya Sheria ya zamani ya Utwaaji Ardhi na sio Sheria mpya ya mwaka 1999 ambayo ilianza kutumika mwaka 2001. Sheria hii mpya inataka malipo ya fidia yalipwe kwa kuzingatia yafutayo:-
(i) Thamani ya ardhi;
(ii) Thamani ya maendelezo;
(iii) Posho za makazi, usumbufu na usafiri; na
(iv) Riba ya kiwango cha soko pale malipo yanapocheleweshwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hukumu hiyo stahili ya wananchi hao ni fidia ya maendelezo, viwanja mbadala na riba ya 6% kwa mwaka mpaka pale malipo yatakapofanyika kama ilivyobainishwa katika Sheria ya Utwaaji Ardhi ya mwaka 1967. Mnamo mwaka 2011 wananchi wa maeneo ya Kipawa na Kigilagila walilipwa fidia yenye wastani wa shilingi bilioni 18. Wananchi wa eneo la Kipunguni bado hawajalipwa fidia zao. Serikali kupitia mamlaka ya viwanja vya ndege ipo katika mkakati wa kutafuta fedha hizo ili kuwalipa wananchi stahiki zao.