Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 28 Energy and Minerals Wizara ya Nishat 234 2016-05-25

Name

Magdalena Hamis Sakaya

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Kaliua

Primary Question

MHE. RIZIKI S. MNGWALI (K.n.y MHE. MAGDALENA H. SAKAYA) aliuliza:-
Wananchi wa Kitongoji cha Twende Pamoja, Kijiji cha Igwisi, Wilaya ya Kaliua wamekuwa wakipata athari kubwa za kiafya kutokana na milipuko ya baruti inayofanywa na Kampuni ya CHIKO, kupasua mawe na kokoto kwa ajili ya ujenzi wa Barabara ya Kaliua mpaka Kigoma:-
(a) Kwa nini Serikali isiwalipe Wananchi hao stahiki zao ili waondoke sehemu hiyo na waende kuishi maeneo mengine ambayo ni salama?
(b) Kijiji cha Igwisi kinanufaikaje na Machimbo haya ya Mawe ambayo yapo kwenye eneo hilo?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Magdalena Hamis Sakaya, Mbunge wa Kaliua, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kampuni ya CHICO inatekeleza mradi wa ujenzi wa barabara wa kilometa 56 kuanzia Kaliua hadi Kazilambwa. Kipande hiki ni sehemu ya barabara kuu inayounganisha wilaya ya Kaliua, Mkoa wa Tabora pamoja na Mkoa wa Kigoma. Ili kupata madini ya ujenzi wa barabara, Kampuni ya CHICO inachimba mawe na kokoto katika leseni ya uchimbaji mdogo PML namba 001290CWTZ iliyopo katika Kijiji cha Igwisi iliyotolewa na Wizara ya Nishati na Madini tarehe 12 Aprili, 2013 kwa TANROADS Tabora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya uchimbaji wa mawe na kokoto inahusisha ulipuaji wa baruti inayoweza kusababisha madhara katika maeneo ya jirani. Ili kuepusha madhara kwa wananchi wanaoishi maeneo hayo, tathmini hufanyika na kwa sasa tathmini ya wananchi 71 imefanyika na kati ya hao, wananchi 34 ni kwa ajili ya mazao na wananchi 37 ni kwa ajili ya makazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kampuni ya CHICO iliwapa fidia waathirika 71 jumla ya shilingi milioni 473.9 chini ya usimamizi wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kupitia TANROADS.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kijiji cha Igwisi kinanufaika na Mradi huu ambapo kwa sasa eneo lao linapitika kwa kipindi cha muda mrefu bila kuwa na matatizo yoyote. Sababu nyingine ambazo zinachangia ni pamoja na kunufaika na uchimbaji huo kwa wannchi kuweza kufanya biashara katika maeneo hayo, lakini pia kwa Halmashauri kulipa service levy. Hivi sasa TANROADS inakusudia kulipa shilingi milioni 23 inachodaiwa kwa kipindi cha Aprili hadi Desemba, 2014.