Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 11 Sitting 49 Works and Transport Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi 646 2023-06-15

Name

Nicholaus George Ngassa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igunga

Primary Question

MHE. NICHOLAUS G. NGASSA aliuliza:-

Je, Serikali inatoa tamko gani kwa mabasi yasiyoingia stendi na ambayo hushusha abiria nje ya stendi?

Name

Atupele Fredy Mwakibete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busokelo

Answer

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Nicholaus George Ngassa, Mbunge wa Igunga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mabasi yote ya masafa marefu hupangiwa ratiba na Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) ambazo huonyesha stendi za kupakia na kushusha abiria pamoja na muda wa kusimama kwenye stendi hizo. Aidha, mabasi ya masafa marefu yamepangiwa kusimama katika stendi moja tu kwa kila Mkoa isipokuwa pale ambapo basi hilo lina abiria anayeshuka katika stendi ya Wilaya. Utaratibu huo umepangwa ili kuondoa usumbufu na ucheleweshaji wa abiria wa masafa marefu kwa kuwalazimisha kuingia kwenye stendi hata kama hawana abiria wa kupanda au kushuka.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Mheshimiwa Ngassa anatoka Igunga, naomba kumtaarifu kuwa, Stendi ya Igunga haimo kwenye stendi ambazo mabasi ya masafa marefu hulazimika kuingia ama kusimama isipokuwa kama yana abiria wa kupanda au kushuka kwenye stendi hiyo. Hata hivyo, stendi hiyo hutumika kwa magari yote yanayotoa huduma ndani ya Mkoa wa Tabora na Mikoa jirani.

Mheshimiwa Spika, kwa madereva wanaokaidi kuingia stendi na kushushia abiria nje ya stendi hususan barabarani, madereva hao wanakiuka maelekezo ya Kifungu cha 50(1) cha Sheria ya Usalama Barabarani, Sura ya 168 kinachomzuia mtu yeyote kuegesha au kusimamisha gari barabarani bila kujali watumiaji wengine wa barabara, hivyo, huvunja Sheria. Ahsante.