Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 34 Good Governance Ofisi ya Rais TAMISEMI. 276 2016-06-01

Name

Sabreena Hamza Sungura

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. AMINA S. MOLLEL (K.n.y. MHE. SABREENA H. SUNGURA) aliuliza:-
Kumekuwa na tatizo kubwa la mgawanyo wa fedha za TASAF ambapo wananchi wengi wasio na uwezo, wamekuwa hawapati fedha hizo.
Je, Serikali imejipangaje kutatua kero hii kwa wananchi ambao hawapati fedha hizo hususan katika Mkoa wa Kigoma?

Name

George Boniface Simbachawene

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibakwe

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (K.n.y. WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sabreena Hamza Sungura, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, utambuzi wa kaya za walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini, ulianza mwezi Novemba, 2013 na hadi sasa umeshaandikisha kaya 1,100,000 katika Halmashauri 159 za Tanzania Bara, pamoja na Wilaya zote za Unguja na Pemba. Kaya hizi zinapata ruzuku kwa utaratibu wa uhaulishaji fedha baada ya kutimiza masharti ya kupeleka watoto shule na kliniki na pia kushiriki katika kazi za kutoa ajira ya muda.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini unaanza ulipanga kufikia asilimia 70 ya Miji, Mitaa na Shehia za Halmashauri ambavyo ndivyo vilivyofikiwa kutokana na mchakato wa kuvipanga, kutokana na viwango vya umaskini katika kila Halmashauri. Baada ya jamii kutambua kaya maskini na kuzipitisha kwenye mikutano ya hadhara iliyosimamiwa na viongozi wa Vijiji, Mitaa na Shehia. Kaya zilizotambuliwa zilijaziwa dodoso ili kukusanya taarifa zaidi za kaya na hatimaye Kaya hizo ziliandikishwa kwenye daftari la walengwa na kuanza kupokea ruzuku.
Mheshimiwa Naibu Spika, ingawa TASAF kwa kushirikiana na Halmashauri ilifanya kila jitihada kuhakikisha kwamba kaya zinatambuliwa na kuandikishwa kwenye mpango ni kaya maskini sana kwenye baadhi ya maeneo Kigoma ikiwa ni mojawapo, baadhi ya jamii na viongozi walifanya udanganyifu na kuingiza majina ya kaya ambazo siyo maskini sana na kuziacha kaya zinazostahili.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuona changamoto hizo, TASAF imefanya mapitio ya orodha ya kaya zilizoandikishwa na kufanya ukaguzi wa nyumba kwa nyumba na kuziondoa kwenye mpango wa kaya zote ambazo siyo maskini. Zoezi hili ni endelevu na ni la kudumu. Kaya zote ambazo siyo maskini na ziliingizwa kwa makosa au kwa makusudi katika orodha ya kaya maskini zitaondolewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka kufikia tarehe 30 Mei, 2016 maeneo yote 161 ya utekelezaji ambayo ni Halmashauri 159 za Tanzania Bara, Unguja na Pemba, zimeshaondoa Kaya ambazo hazistahili kuwemo kwenye orodha ya walengwa. Jumla ya kaya 25,446 zimeshaondolewa kwenye mpango kwa sababu mbalimbali ikiwemo vifo, kukosa vigezo vya kaya maskini na kuondolewa kwa Wajumbe wa Kamati za Mpango na viongozi wa Vijiji na Mtaa na Shehia katika orodha ya kaya maskini.