Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 11 Sitting 54 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 712 2023-06-23

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Primary Question

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU aliuliza: -

Je, ni lini mianya ya majadiliano yanayopelekea rushwa kwenye mfumo wa ukadiriaji wa kodi kwa Wafanyabiashara itaondolewa?

Name

Hamad Hassan Chande

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kojani

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Constantine John Kanyasu, Mbunge wa Geita Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ukaguzi na makadirio ya kodi huongozwa na Sheria ya Usimamizi wa Kodi, Sura 438 na Kanuni zake, pamoja na miongozo inayotolewa na Serikali kupitia TRA. Hivyo, mawasiliano yote yanayofanyika baina ya TRA na Mlipakodi kabla ya makadirio ya kodi kutolewa yanaongozwa na misingi iliyotajwa hapo juu. Aidha, TRA inachukua hatua mbalimbali ili kuondoa mianya ya rushwa kama ifuatavyo: -

(i) Kutoa elimu kwa walipa kodi kujua haki na wajibu wao;

(ii) Kuimarisha usimamizi wa sera ya maadili kwa watumishi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania;

(iii) Kurahisisha utoaji wa taarifa za watumishi wanaojihusisha na vitendo vya rushwa kupitia tovuti na kupiga simu kupitia namba za simu zisizo na gharama; na

(iv) Kushirikiana na taasisi mbalimbali za Serikali katika kuelimisha, kuzuia na kushughulikia vitendo vya ukiukwaji wa maadili ndani ya mamlaka.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania inaendelea kuunda, kutumia na kuimarisha utendaji kazi wa mifumo mbalimbali ya TEHAMA ili kupunguza vitendo vya ubadhilifu na rushwa vinavyosababishwa na utaratibu wa kuonana ana kwa ana kwa Afisa wa Kodi na Mlipa Kodi wakati wa ukadiriaji wa mapato. Ahsante.