Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Atupele Fredy Mwakibete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busokelo

Primary Question

MHE. ATUPELE F. MWAKIBE aliuliza: - Je, lini Mkataba wa Ujenzi wa Barabara ya Katumba – Mbambo hadi Tukuyu utasainiwa kwa kuwa Mkandarasi alishapatikana?

Supplementary Question 1

MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina swali moja la nyongeza. Kwanza namshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa ujenzi wa barabara hii kwa kilomita 27 na sasa bado kilomita 56. Je, ni lini hizi kilomita zilizobaki zinakwenda kusainiwa ukizingatia kwamba Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi kaka yangu Innocent Bashungwa pamoja na Mheshimiwa Waziri wa Fedha walitembelea Jimbo la Busokelo tarehe Mosi Oktoba na walifanya mkutano mzuri sana. Tunawashukuru sana kwa kuja, ninyi ni mashuhuda wazuri kwamba barabara hii inahitaji kujengwa kwa kiwango cha lami. Je, ni lini itasainiwa? (Makofi)

Name

Innocent Lugha Bashungwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Karagwe

Answer

WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwanza nampongeza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri pia nampongeza Mheshimiwa Mwakibete kwa kuupiga mwingi kwa ajili ya wananchi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara anayoitaja Mheshimiwa Mwakibete ni moja ya barabara 15 ambazo tunasubiri kusaini. Nawapongeza Waheshimiwa Wabunge wote wa barabara hizi, Mheshimiwa Rais ameshatoa kibali kama Mheshimiwa Naibu Waziri alivyosema. Tumeona tuandae siku ambayo tutasaini mikataba hii kwa siku moja halafu baada ya hapo mimi pamoja na Mheshimiwa Naibu Waziri tutaambatana na Waheshimiwa Wabunge kwenda kuwakabidhi wakandarasi kwenye Majimbo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba Waheshimiwa Wabunge, tuko mbioni katika kuandaa tukio hili ambalo tutaomba Kiongozi Mkuu wa Kitaifa aweze kushuhudia utiaji saini huu. Nawapongeza sana Waheshimiwa Wabunge, sasa tunaenda kufanya kazi na miradi hii 15 ina thamani ya shilingi 1,034,000,000. Natumia nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais na Waheshimiwa Wabunge wamefanya kazi kubwa ya ufuatiliaji. Tumefika hatua nzuri na Serikali ya Awamu ya Sita hakika katika kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi imejipanga vizuri, ahsante. (Makofi)