Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Primary Question

MHE. MASHIMBA M. NDAKI aliuliza: - Je, Mkandarasi wa SGR kipande cha Seke-Malampaka hadi Malya ameajiri wananchi wangapi wanaotoka maeneo hayo?

Supplementary Question 1

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa kuna malalamiko kwamba hata kazi ndogo ndogo kama za usafi, kufyeka na ulinzi, mkandarasi anatoa wafanyakazi maeneo ya mbali badala ya maeneo ya Seke, Malampaka na Malya. Je, Serikali inamshauri nini mkandarasi huyu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa pia kuna malalamiko kwamba mkandarasi ambaye ndiyo mwajiri hapeleki au anapeleka michango kwenye Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kwa kusuasua, je Serikali inasemaje juu ya malalmiko haya? (Makofi)

Name

David Mwakiposa Kihenzile

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mufindi Kusini

Answer

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mashimba Mashauri Ndaki.

Mheshimiwa Spika, la kwanza, amezungumzia kuhusiana na watu wengi kutoka nje ya eneo la mradi. Moja, nimetoa takwimu ya watu ambao wameajiriwa kutoka kwenye eneo hilo katika Mkoa wake wa Shinyanga.

Pili, nimkumbushe tu Mheshimiwa Mbunge kwamba mradi huu ni wa Kitaifa. Hata hivyo, Serikali itaendelea kumsimamiwa na kumsisitiza kwamba, anatafuta kwanza wafanyakazi kwenye eneo husika kabla hajepeleka kipaumbele kwenye maeneo mengine ya nje ya eneo husika.

Mheshimiwa Spika, hoja yake pili ni kuhusiana na michango ya NSSF, kwamba pengine mkandarasi anasuasua. Tunafahamu Sheria ya NSSF (The National Social Security Act) Revised ya 2018 Cap. 50, inamtaka mkandarasi au mwajiri kuhakikisha kwamba anapeleka makato hayo NSSF mapema iwezekanavyo.

Mheshimiwa Spika, tunatambua kwamba kuna changamoto kubwa sana kwenye upande wa mkandarasi huyu kwa sasa. Tayari tumeshaanza vikao kupitia wenzetu Ofisi ya Waziri Mkuu, kwa ajili ya kukaa naye na kuweka commitment, mara tu anapolipwa fedha aweze kupeleka michango hiyo kwenye Mifuko ya Hifadhi za Jamii. Pia, aweze kuwalipa na wazabuni mbalimbali wa ndani. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, naona umesimama.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri, napenda tu kuongezea kwenye kile kipengele cha mkandarasi kutopeleka michango kwenye Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF).

Mheshimiwa Spika, nakiri kweli kuna madai ambayo mkandarasi anadaiwa na Mfuko umekuwa ukifatilia madai hayo na kuna makubaliano ambayo NSSF imeweka na mkandarasi ambapo tunataka madeni haya yakamilike ndani ya mwaka mmoja.

Mheshimiwa Spika, nimesimama pia kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba, kuna utaratibu ambao umewekwa kati ya NSSF na mkandarasi kwa wale ambao wanatakiwa kulipwa mafao yao sasa, kuna utaratibu maalum wa fedha zao kupatikana ili wasiathirike na malipo hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nikuhakikishie kwamba, kama Wizara ambayo tunasimamia mifuko ya hifadhi ya jamii, tutahakikisha kwamba madeni haya tunayafatilia ili haki za wafanyakazi zisipotee. Ahsante sana.