Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Aida Joseph Khenani

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Nkasi Kaskazini

Primary Question

MHE. AIDA J. KHENANI aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kupitia upya mipaka ya hifadhi na makazi ya wananchi Wilayani Nkasi?

Supplementary Question 1

MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, pamoja na majibu ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; mipaka hii ambayo inazungumzwa leo iliwekwa mwaka 1948. Ukiangalia idadi ya watu ilikuwa ni watu wachache kuliko ilivyo leo. Kwa kuwa hii migogoro imekuwa ya muda mrefu na ilisababisha tamko na maagizo ya Waziri Mkuu hapa Bungeni kwa Wizara ya Maliasili na Utalii kuja Nkansi kupitia upya mipaka hiyo kwa kushirikiana na TAMISEMI, mpaka leo hamjafika. Ni lini mtatekeleza agizo la Waziri Mkuu alilotoa kupitia Bunge lako tukufu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; pamoja na changamoto ya migogoro iliyopo kwenye hii mipaka, lakini bado tembo wamekuwa wanavuka kutoka kwenye eneo lao la pori tengefu kwenda kwenye makazi ya wananchi na kula mazao na kuvamia makazi na hivi sasa hawana chakula tena.

Ni lini mtawalipa wananchi hawa kwa kuangalia hali halisi ya sasa badala ya kufuata sheria ya wanyamapori ambayo inawaumiza wananchi wetu? (Makofi)

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Aida Khenani, Mbunge wa Nkansi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Pori la Akiba la Rwafi ni pori ambalo kabla ya kuanzishwa lilikuwa chini ya Halmashauri. Baada ya Halmashauri kushindwa kulisimamia vizuri lililetwa katika Wizara ya Maliasili na Utalii na wakati huo huo wananchi walikuwepo ambao walikuwa hawaijui mipaka vizuri na wakahitaji kufafanuliwa mipaka.

Mheshimiwa Spika, hivi sasa ninavyoongea zaidi ya kilometa 50 tayari zimeshaanza kuoneshwa kwa maana ya kuwekwa vigingi kwa kushirikisha wananchi. Kwa hiyo, nimuombe tu Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa kuwa zoezi hili linaendelea, wataalamu wataendelea kushirikisha wananchi kuonesha mipaka halisi ya pori hilo ili waweze kutambua maeneo ambayo yamehifadhiwa.

Mheshimiwa Spika, na swali hili la pili kuhusiana na tembo, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Nkansi kwamba kwa kuwa Serikali imeendelea kulipa kifuta machozi na kifuta jasho, nimtaarifu tu Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Nkansi tutaenda kulipa kifuta machozi kabla ya kuisha mwaka huu wa fedha, ahsante.

Name

Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Primary Question

MHE. AIDA J. KHENANI aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kupitia upya mipaka ya hifadhi na makazi ya wananchi Wilayani Nkasi?

Supplementary Question 2

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa fursa ya swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, na mimi nilitaka kujua ni lini Serikali itatatua mgogoro kati ya Hifadhi ya Kitulo na wananchi wa Kijiji cha Kikondo, Kata ya Ilungu ambao ni
wa muda mrefu na viongozi wetu wa kitaifa walishatoa ahadi ya kutatua huo mgogoro na kisha wananchi walipwe fidia? Ahsante.

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oran Njeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli Hifadhi ya Kitulo ina changamoto, kuna migogoro kati ya hifadhi na maeneo ya wananchi, lakini zoezi hili liliingizwa kwenye Kamati ya Mawaziri Nane na hivi ninavyoongea baada ya Bunge hili kuisha, zoezi hili litaendelea kwenda kutoa ufafanuzi katika maeneo yaliyobaki ikiwemo Mkoa wa Iringa na Njombe ambapo kamati hii haijafika. Hivyo, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba zoezi hili tunaenda kulitekeleza, tutaenda kutatua migogoro hii na wananchi waweze kuishi kwa amani.

Name

Justin Lazaro Nyamoga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilolo

Primary Question

MHE. AIDA J. KHENANI aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kupitia upya mipaka ya hifadhi na makazi ya wananchi Wilayani Nkasi?

Supplementary Question 3

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, katika Kata ya Image na Kata ya Ibumu, Kijiji cha Ilambo na Iyai kuna changamoto kubwa ya mipaka na kusababisha wananchi mara nyingi kugongana kwenye malisho.

Je, Wizara ina mpango gani wa kufika katika maeneo hayo na kutatua mgogoro huo?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Justin Lazaro, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nimuahidi tu Mheshimiwa Mbunge na wananchi wake kwamba nitaenda mimi mwenyewe kufanya ziara na kuzungumza na wananchi na kutatua changamoto hii.

Name

Daniel Awack Tlemai

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Karatu

Primary Question

MHE. AIDA J. KHENANI aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kupitia upya mipaka ya hifadhi na makazi ya wananchi Wilayani Nkasi?

Supplementary Question 4

MHE. DANIEL A. TLEMAI: Mheshimiwa Spika, ahsante, Kata ya Endamaghang na Kijiji cha Endamaghang kuna mgogoro uliodumu muda mrefu na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro toka mwaka wa 2003. Sasa ni lini Serikali itaweza kutatua mgogoro huo ambao umedumu tangu mwaka 2003 mpaka leo hii?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Daniel Awack, Mbunge wa Karatu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tuna migogoro mipya na migogoro ambayo Kamati ya Mawaziri Nane inaendelea kuitatua. Kwa hii migogoro mipya nimuahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tumeendelea kuhamasisha maeneo yote ambayo yana migogoro hii tuanze pia kuyapitia upya na kuyatolea ufafanuzi ikiwemo kutatua au kutafsiri mipaka kati ya ramani za vijiji na ramani za hifadhi.

Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge tutafika katika eneo lake ili tuweze kutoa ufafanuzi na pale ambapo itaonekana ramani zimeingiliana, basi Wizara ya Ardhi watatatua changamoto hii na tutaendelea kuhifadhi maeneo yaliyohifadhiwa.

Name

Anne Kilango Malecela

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Same Mashariki

Primary Question

MHE. AIDA J. KHENANI aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kupitia upya mipaka ya hifadhi na makazi ya wananchi Wilayani Nkasi?

Supplementary Question 5

MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, nashukuru na nakiri kwamba Mheshimiwa Waziri alishakuja jimboni kwangu akaona matatizo ya Kata yangu ya Mahoro, Kalemawe na Ndungu, lakini zaidi ya wananchi 300 ambao mazao yao yamevurugwa sana kwenye mashamba na hawana chakula sasa hivi hawajalipwa chochote tangu mwaka 2021. Na wananchi wangu wawili wameuawa na tembo, hawajalipwa chochote tangu mwaka 2021, Mheshimiwa Waziri nitakuletea list yote leo; je, unaniahidi utawalipa lini?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anne Kilango, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge, hivi ninavyoongea sasahivi hapa nikitoka hapa tu naenda kufuatilia, ili wananchi wa Same waweze kulipwa madai yao ya kifuta machozi na kifuta jasho. (Makofi)

Name

Philipo Augustino Mulugo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songwe

Primary Question

MHE. AIDA J. KHENANI aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kupitia upya mipaka ya hifadhi na makazi ya wananchi Wilayani Nkasi?

Supplementary Question 6

MHE. PHILLIPO A. MULUGO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kuniona, naomba niiulize Serikali kwa kuwa Tume ya Mawaziri Nane haijawahi kufika Songwe na nimekuwa nikielezea hili jambo kila wakati.

Je, Tume hiyo baada ya kumaliza Bunge, iko radhi kufika Songwe katika Vijiji vya Gua, Nangwala, Kapalala, Udinde, Mkwajuni, Patamela, Saza na Mbangala kwa ajili ya kulinda mipaka ile ya maliasili, hasa TANAPA, TAWA na TFS katika maeneo ya wachimbaji wadogo?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mulugo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa mzungumzaji hajasema kama hivyo vijiji vina migogoro, nimhakikishie tu kwamba vile ambavyo viko ndani ya Kamati ya Mawaziri Nane, Kamati ya Mawaziri Nane watafika bila kuchelewa, lakini kama ni migogoro mipya tunaiomba ili tuweze kuiingiza kwenye orodha ya migogoro mipya ili tuandae tena utaratibu wa kwenda kushughulikia migogoro hiyo, ahsante.

SPIKA: Mheshimiwa Deus Sangu, swali la nyongeza.

Ngoja Mheshimiwa Deus Sangu, Mheshimiwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa kunipa fursa, kwanza nishukuru kwa majibu mazuri aliyoyatoa Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Spika, napenda tu niwafahamishe Waheshimiwa Wabunge kwamba ile Kamati ya Kisekta ya Mawaziri Nane, Wizara ya Ardhi ndio Mwenyekiti wa Kamati hiyo. La msingi tunalofanya si kwamba tutafika kila Kijiji, ni kwamba majukumu haya pia tunawapa mikoa ambayo ndio wanajua maeneo yao vizuri. Na sisi tunapokwenda tunazungumza na mikoa, wanatoa programu yao, pale ambapo wanakuwa wanahitaji uongozi wa ngazi za Wizara ndipo tunakwenda, lakini majukumu yote yanabebwa na mikoa husika kama mamlaka za utawala katika maeneo yale.

Name

Deus Clement Sangu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwela

Primary Question

MHE. AIDA J. KHENANI aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kupitia upya mipaka ya hifadhi na makazi ya wananchi Wilayani Nkasi?

Supplementary Question 7

MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa fursa ya swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, nataka muuliza Mheshimiwa Naibu Waziri; je, ni lini mtamaliza mgogoro uliopo kati ya Kata ya Nankanga, Kipeta na Kilangawani kwa Pori la Akiba lile la Uwanda na wewe mwenyewe ulikuja ukajionea mgogoro ule ambavyo unawatesa wananchi? (Makofi)

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deus Sangu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli nilifika katika eneo hili ambapo kulikuwa kuna changamoto kati ya hifadhi kwa maana ya maeneo ya Ziwa Rukwa pamoja na wananchi wanaoishi maeneo hayo. Lakini nimuombe tu Mheshimiwa Mbunge kwamba ufafanuzi tuliutoa na tutaendelea kuutoa, na tutafika pale kuendelea kutoa ufafanuzi kwa sababu maeneo yale tunayahifadhi kwa ajili ya kuzuia wavuvi kusogea kwenye maeneo ambayo ni mazalia ya samaki.

Mheshimiwa Spika, wananchi wengi wanataka wafike wavue kwenye maeneo ambayo mwisho wa siku watajikuta wanakosa mazao ya samaki. Hivyo, hata wananchi tunapaswa kuwaeleza ukweli kwamba kuna maeneo ambayo yanahifadhiwa kwa ajili ya faida yao wenyewe. Tutafika, tutatoa ufafanuzi, lakini wananchi wanatakiwa wafahamu tunatunza kwa ajili ya matumizi ya wao wenyewe wananchi, ahsante.

Name

Dr. Charles Stephen Kimei

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vunjo

Primary Question

MHE. AIDA J. KHENANI aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kupitia upya mipaka ya hifadhi na makazi ya wananchi Wilayani Nkasi?

Supplementary Question 8

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali langu ni kuhusu Nusu Maili; Nusu Maili ambayo ni eneo la Nusu Maili kuanzia vijiji kwenda kwenye hifadhi inayozunguka Mlima Kilimanjaro liliwekwa mwaka 1923 na Serikali za wakoloni.

Naomba nijue kwamba hii Kamati ya Mawaziri Nane imefikia muafaka gani kuhusu hilo eneo kwa sababu kuna mkanganyiko mkubwa sana kuhusiana na maagizo ya Waziri aliyekuwepo Mheshimiwa Jumanne Maghembe na hali ilivyo sasa hivi?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuna maeneo ambayo tunatamani sana wananchi wafahamu kwamba ni maeneo ya muhimu. Eneo hili la Nusu Maili ni eneo ambalo tumeukinga Mlima Kilimanjaro ili barafu yake isiendelee kuyeyuka. Tumeendelea kuwaelimisha wananchi namna ambayo tunaweza tukafanya kama ni mbadala, badala ya kuendelea kuomba Nusu Maili, sisi tumejipanga kugawa miche kwa ajili ya wananchi wapande miti ili iweze kuwasaidia baadae kuwa na mavuno ya zao la miti ikiwemo kupata mkaa na matumizi ya nishati mbadala.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niendelee kuwaomba wananchi wanaozunguka Mlima Kilimanjaro. Mlima Kilimanjaro tunapata faida kubwa sana ikiwemo kupata watalii na hata wenyeji walioko katika maeneo hayo wanafaidika ikiwemo sisi kupeleka CSR kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, hii Half Mile ambayo tumeendelea kuiomba tuwaombe kwamba Mlima Kilimanjaro unahitaji kuhifadhiwa vizuri kwa ajili ya kizazi hiki na vizazi vinavyokuja. Kwa hiyo, niwaombe wananchi wanaozunguka Mlima Kilimanjaro tuendelee kushirikiana na Serikali kuutunza mlima huu.