Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Aysharose Ndogholi Mattembe

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati Hospitali ya Wilaya ya Manyoni?

Supplementary Question 1

MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza kabisa naipongeza Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kusikia kilio chetu na kuikarabati Hospitali ya Wilaya ya Manyoni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto kubwa kwa sasa ni ukosefu wa vifaa tiba.

Je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kupeleka vifaa tiba vya kutosha hususan katika Jengo la Mama na Mtoto?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa hospitali hii inakabiliwa na uhaba wa watumishi, ningependa kujua, ni upi mkakati wa Serikali wa kuwapatia watumishi 169 ili kuendana na mahitaji yaliyopo?

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Aysharose Mattembe kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ameendelea kujali afya za Watanzania na kupeleka fedha nyingi katika halmashauri zetu kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya huduma za afya. Sambamba na hilo, vifaa tiba vimeendelea kupelekwa katika vituo vilivyokamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba Halmashauri ya Manyoni na hospitali hii imeshapokea zaidi ya shilingi milioni 750 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba. Bado Serikali itaendelea kupeleka fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunakuwa na vifaa tiba vya kutosha zaidi katika Jengo la Mama na Mtoto na katika majengo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili kuhusiana na upungufu wa watumishi, Serikali imeendelea kuajiri watumishi kwa awamu na kuwapangia katika halmashauri kote nchini ikiwemo Halmashauri hii ya Manyoni. Nimhakikishia kwamba tunatambua kuna upungufu wa watumishi hawa na Serikali itaendelea kuajiri kwa awamu kuhakikisha kwamba watumishi wanapelekwa katika hospitali hii, ahsante. (Makofi)