Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Maimuna Ahmad Pathan

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MAIMUNA A. PATHAN aliuliza:- Je, kwa nini Serikali isifanye utaratibu wa kwenda kuhakiki wastaafu kwenye Wilaya zao kuliko ilivyo sasa kuhakikiwa mikoani?

Supplementary Question 1

MHE. MAIMUNA A. PATHAN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Nataka kujua, hilo suala la kuwafuata Wilayani au mahali popote walipo lilianza lini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, kama tunavyojua, ukistaafu umeshakuwa mtu mzima, afya nayo mara nyingi inadorora na uchumi unakuwa chini; nina ombi kubwa sana Serikalini. Kulingana na majibu ya swali la msingi, naomba Serikali ifanye hivyo, kwa sababu utakuta kuna mtu anatoka sehemu inaitwa Kandawale yenye kilometa 309 kutoka Mkoani, mtu mwingine anatoka Kimambi zaidi ya kilometa 290, kutoka Mkoani; naomba Serikali ijitahidi kufanya huo utaratibu ambao imeusema kwa kuwafuata hata kama ni kwenye Tarafa ili kuwapunguzia adha ya usafiri kulingana na uchumi wao na afya zao, kwa sababu tayari ni watu wazima, ahsante sana. (Makofi)

Name

Paschal Katambi Patrobas

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Shinyanga Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari mfuko umeshaanza utaratibu wa kimtandao na mwanachama anaweza kujihakiki kwa kupitia biometric verification ambayo hiyo itaenda kuweka kwenye maeneo hayo. Ukiangalia kwenye tovuti, tayari inaeleza utaratibu wa kuitumia. Mbali na biometric verification, tuna member portal, yaani mwanachama anakuwa na account yake maalum kwenye tovuti ambapo anaweza akaingia na kuhakiki taarifa zake kwa kupitia mfumo huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, tuna mfumo mwingine wa uhakiki wa vidole ambao utaenda kwenye Halmashauri zote. Kwa hiyo, mwanachama anafika kwenye halmashauri yake kwa sababu ni eneo la karibu na anaweza akaweka kidole chake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini tunafanya uhakiki? Umuhimu wa uhakiki, kwanza ni kwa sababu lazima tuwe na uhakika wa watu wanaolipwa ndiyo sahihi wanaostahili. Kwa sababu kuna kipindi ilitokea kukawa na watu wanafanyiwa malipo hewa, wanachama walishafariki, mnajikuta malipo yanaendelea kulipwa na hii kupelekea hasara katika mfuko. Kwa hiyo, verification inasaidia sana katika kuhakiki kwanza uanachama wake na pia, kuweza kuboresha na kuangalia stahili zake nyingine.