Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Innocent Edward Kalogeris

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Primary Question

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS aliuliza: - Je, lini Halmashauri ya Morogoro Vijijini na Rufiji zitalipwa fedha za CSR kwa ajili ya ujenzi wa mradi wa kuzalisha umeme wa Julius Nyerere?

Supplementary Question 1

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama za ujenzi katika Mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere ni takribani trilioni 6.5 na CSR ambayo inatakiwa kulipwa kwa Halmashauri ya Morogoro Vijijini na Halmashauri ya Rufiji ni takribani bilioni 276. Siku za nyuma Serikali kupitia Wizara ilitaka fedha hizo za CSR za ujenzi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere ziende zikajenge Uwanja wa Mpira Dodoma. Mkandarasi alikataa kwa sababu, utaratibu wa mkataba unakataza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika Bunge hilihili katika Taarifa iliyoletwa na Kamati ya Bajeti ilisema kwamba, fedha za CSR zinataka kwenda kujenga Chuo cha TEHAMA Kigoma bilioni 80, kujenga Chuo cha Gesi Asili ya Lindi bilioni 80, lakini kujenga vyuo vya utabibu Dodoma na Tanga bilioni 80. Juzi Mheshimiwa Rais wakati anasimamia uitiaji saini wa vitalu vya gesi alisema, fedha za CSR ziendelee kunufaisha wananchi katika maeneo husika na sababu za kunufaisha wananchi katika maeneo husika ni kwamba kwanza wananchi wale ni walinzi wa mradi, lakini wananchi wale ni waathirika kwa sababu, kuna mahali kushoto au kulia wanakosa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa swali; hizi fedha bilioni kumi-kumi ambazo tunapewa Halmashauri ya Morogoro Vijijini kwa ajili ya ujenzi wa hospitali yenye hadhi ya Wilaya katika Kata ya Kisaki na Wananchi wa Rufiji katika Kata ya Nyamwage ni nini? Ni sehemu kwamba, bado tutaendelea kupata fedha katika mradi huu au ndio zimekwisha? Na kama zimekwisha, Serikali inasema nini kwa Wananchi wa Halmashauri ya Morogoro Vijijini na wananchi wa Halmashauri ya Rufiji kuhusu fedha yao hii ambayo ni haki Kikatiba, je, kuna double standard katika nchi hii katika CSR, kwamba kuna wengine wanapewa wengine hawapewi? (Makofi)

Name

Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa naba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali moja la Mheshimiwa Kalogeris, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitumie fursa hii kusema kwamba Serikali inaelewa concerns za Wabunge wa Morogoro na Pwani. Jambo hili limekwishafika Serikalini, Mkuu wa Mkoa wa Pwani alitufikishia, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro alitufikishia na hata kwenye Kamati ya Nishati jambo hili lilifikishwa, itoshe kusema jambo hili ni la kimkataba, hizo changamoto zilizojitokeza tumeziona, Serikali inafanyia kazi changamoto hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ipo tayari kwa kushirikisha wadau wote wanaohusika na jambo hili, kupitishana kwenye yale ambayo tunayafanyia kazi ili mwisho wa siku tuweze kupata ufumbuzi wa pamoja. Namuomba Mheshimiwa Mbunge awe na Subira, Serikali imeelewa na tupo tayari kulifanyia kazi. (Makofi)