Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Stanslaus Shing'oma Mabula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nyamagana

Primary Question

MHE. STANSLAUS S. MABULA K.n.y. MHE. SIMON S. LUSENGEKILE aliuliza: - Je, ni lini barabara ya Nyashimo – Ndutwa – Shigala – Malili hadi Ngasamo itajegwa kwa kiwango cha lami?

Supplementary Question 1

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Swali la kwanza, kwa kuwa kumekuwa na utaratibu wa Serikali kufanya upembuzi yakinifu na unapokamilika barabara zinachukua muda mrefu, barabara hii ni muhimu sana kwa wananchi wa Wilaya ya Busega, Wilaya za Nyashimo, Ndutwa na Ngasamo na maeneo mengine kuunganisha na Mkoa wa Simiyu kwa maana ya Mkoani. Ni nini sasa kauli ya Serikali kuhakikisha kwamba pindi tu upembuzi yakinifu utakapokuwa umekamilika barabara hii itajengwa? (Makofi)

Swali la pili, barabara kuu itokayo Mwanza Mjini kwenda Shinyanga kupitia maeneo ya Igogo – Mkuyuni – Buhongwa – Usagara ambayo imeshafanyiwa upembuzi yakinifu takribani miaka miwili sasa imepita, kwa kweli Mji umebanana sana. Ningependa kujua sasa kauli ya Serikali, ni lini barabara hii itajengwa kwa kiwango cha njia nne na kuondoa usumbufu uliopo sasa? (Makofi)

Name

Eng. Godfrey Msongwe Kasekenya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ileje

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni utaratibu wa kawaida kwamba kabla barabara haijaanza kujengwa kwa kiwango cha lami, tunatakiwa tufanye upembuzi yakinifu na usanifu wa kina, hii inaisaidia Serikali kuweza kujua gharama ya hiyo barabara. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, ukishafanya usanifu inakusaidia hata kama ni wahisani ama Serikali inakuwa kwenye nafasi ya kuweza kuipangia bajeti. Kwa hiyo, kuifanyia usanifu maana yake ni mpango wa Serikali kuijenga kwa kiwango cha lami kwa sababu ni kweli hiyo barabara ni muhimu sana kwa wananchi wa Busega.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili la barabara kubwa, barabara kuu ya kutoka Mwanza – Mkuyuni – Buhongwa – Usagara ambayo inakwenda mpaka kati ya mpaka wa Mwanza na Shinyanga, barabara hii iko kwenye mpango wa kuijenga njia nne. Tumeshakamilisha usanifu. Ni mradi mkubwa na tunajua Mwanza sasa ni Jiji kubwa ambalo foleni ni kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali imeweka kwenye mpango barabara hii, kutafuta fedha kuijenga barabara yote kwa njia nne kwa kiwango cha lami, ahsante.