Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Mwanaisha Ng'anzi Ulenge

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE aliuliza:- Je, kuna mkakati gani wa kufufua viwanda vilivyokufa katika Mkoa wa Tanga?

Supplementary Question 1

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la kwanza ni kwamba Sheria ya Kodi na Sheria za Uwekezaji hazisomani, kwa maana miradi mingi inafunguliwa lakini wawekezaji hawafanyi hivyo kwa sababu hakuna vivutio. Je, ni lini Serikali italeta hapa sheria hizo ili ziweze kupitiwa upya na ziweze kusomana? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili. Shirika la UNDP limewezesha mikoa mbalimbali kuanzisha miongozo ya uwekezaji, na kule Tanga tumeanzisha na tumeanza kuzindua miongozo ile ya uwekezaji. Ni nini sasa Serikali inafanya baada ya miongozo ile kuenea Tanzania nzima ili dhamira ile ya kuanzisha viwanda iweze kutimia? (Makofi)

Name

Exaud Silaoneka Kigahe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mufindi Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli bado kuna changamoto kwenye baadhi ya sheria na pia kwenye sera za uwekezaji. Serikali imeishaanza kupitia sheria mbalimbali za taasisi zetu, sheria za kodi, na vile vile tumeanza kuboresha au kuhuisha sera zetu mbalimbali ikiwemo Sera ya Uwekezaji, Sera ya Viwanda na Sera ya Biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, haya niliyosema ndiyo ambayo Serikali tunafanya sasa ili kuhakikisha sera zetu na sheria zetu zinaendana na mahitaji sahihi kulingana na uhalisia wa sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kama nilivyosema, tumeshaanza kutengeneza miongozo mbalimbali ya uwekezaji na miongozo hii au makongamano haya yamekuwa yakifanyika katika mikoa mbalimbali ikiwemo Mkoa wa Tanga. Matokeo haya katika Mkoa wa Tanga mahususi ni kutengwa kwa maeneo. Kwa mfano, maeneo yale kongwe ya maeneo ya uwekezaji 68, haya yamewekwa kwa ajili ya kujenga viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, miongozo hii sasa imeshaanza kuzaa matunda, na wawekezaji wengi wameshaanza kuonesha nia ya kuwekeza katika nchi yetu, na pia katika Mkoa wa Tanga ambako Mheshimiwa Mbunge ameuliza. Nakushukuru sana.

Name

Shally Josepha Raymond

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE aliuliza:- Je, kuna mkakati gani wa kufufua viwanda vilivyokufa katika Mkoa wa Tanga?

Supplementary Question 2

MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Naibu Spika, sana. Jibu la Serikali linatia matumaini. Naomba kufahamu katika mwendelezo huo wa kufufua viwanda, je, Viwanda vya Losaa Kilimanjaro, Kilimanjaro Machine Tools, Moshi Leather na Kilimanjaro Utilization viko katika mpango huo? Ahsante.

Name

Exaud Silaoneka Kigahe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mufindi Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli katika mikakati ambayo tumeiweka ni pamoja na kufufua viwanda. Kiwanda hiki cha Losaa ambacho tayari tumeshapeleka Shirika letu la Maendeleo ya Viwanda Vidogo Tanzania (SIDO), wameshaenda kufanya tathmini ya namna ya kufufua kiwanda kile.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Kilimanjaro Machine Tools tayari tumeshaweka mitambo mipya mbalimmbali ambayo inafanya kazi, na tunaendelea kuongeza kwa kuweka bajeti katika mwaka huu ili kununua mitambo mingine ya kuyeyusha chuma katika kuhakikisha vipuri mbalimbali vinatengenezwa katika viwanda hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, tunaenda hatua kwa hatua kuhakikisha kuwa viwanda vyote ambavyo vilikuwa vimekufa vinafufuliwa na hasa katika Mkoa wa Kilimanjaro. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Waziri wa Mipango, Ofisi ya Rais.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka tu niongezee kwenye majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri pale kwa Mheshimiwa Eng. Ulenge kwamba, sasa hivi katika reform za Mashirika ya Umma, tunaunganisha taasisi ambazo zinahusika na uwekezaji kwa maana ya TIC na EPZA. Kwa kufanya hivyo, tutazipitia upya sheria zote husika na yale Mheshimiwa Mbunge aliyoyasema tutayaangalia. Nashukuru sana. (Makofi)