Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Husna Juma Sekiboko

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO K.n.y. MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU aliuliza:- Je, lini watumishi wa umma watarekebishiwa madaraja hasa walimu waliopandishwa na kunyang’anywa mwaka 2016 - 2018 kupisha uhakiki?

Supplementary Question 1

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa uhakiki umefanyika tangu mwaka 2018 lakini wapo walimu mpaka leo wanadai malipo yao kulingana na madaraja ambayo wamepandishwa bila impact kwenye mishahara yao, ni ipi kauli ya Serikali juu ya walimu wenye madai haya?

Mheshimiwa Naibu Spika, wapo watumishi katika kada mbalimbali ambao wamekuwa wakidai arrears kwa miaka mingi zaidi ya miaka mitano, je, Serikali ina mpango gani wa kukamilisha madeni haya ya watumishi?

Name

Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Husna Sekiboko anayeuliza kwa niaba ya Mheshimiwa Jesca Jonathani Msambatavangu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kulipa madai mbalimbali ya mishahara, lakini pia madai mbalimbali ya madeni ambayo yaliachwa kutokana na zoezi linaloendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, Bunge lako lilitoa maelekezo kwa Serikali na Serikali ilifanya utaratibu wake wa kuwajulisha waajiri wote walete taarifa za watumishi wote ambao wana madai kwenye Serikali yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka huu wa fedha tumetenga nafasi 52,551 kwa ajili ya kwenda kulipa madeni yote ambayo watumishi wanadai ambayo tayari yamehakikiwa. Kwa wale ambao hawajaleta madai ya watumishi wetu katika maeneo mbalimbali, msisitizo wangu katika asubuhi ya leo, ni kuendelea kuwakumbusha tena waajiri wote leteni madeni tunayodaiwa kwa sababu hii ni haki ya watumishi wa umma kulipwa na Serikali yao inayoongozwa na Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Bunge lako lilitupitishia bajeti na kwa kweli tunakushukuru wewe Naibu Spika kwa niaba ya Bunge na nataka niwahakikishie watu wote ambao madeni yao hayajalipwa, nataka nirudie tena, waajiri leteni taarifa zao na Serikali ipo tayari kwa ajili ya kuyalipa madeni yote.