Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Mohammed Said Issa

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Konde

Primary Question

MHE. MOHAMED SAID ISSA aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kuleta unafuu wa gharama za michango ya kujiunga na masomo ya kidato cha kwanza na cha tano?

Supplementary Question 1

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, je, Serikali ipo tayari kuainisha aina ya michango hiyo ambayo imeruhusiwa kuombewa kibali?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, je, Serikali ipo tayari kutoa maelekezo kwa Wakuu wa Shule kuwaruhusu wanafunzi ambao hawana uwezo wa kuchangia michango hiyo kwa wakati? Nakushukuru. (Makofi)

Name

Zainab Athuman Katimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. ZAINAB A. KATIMBA): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kama nilivyojibu kwenye majibu yangu ya msingi, Waraka wa Elimu Na. 3 wa mwaka 2016 umeeleza na umeweka utaratibu wa kuzingatiwa ili kuweza kupata kibali kwa ajili ya kuwepo kwa michango katika shule za msingi lakini katika shule za sekondari iwapo kuna uhitaji na katika waraka huo ni lazima kupata kibali cha Mkuu wa Wilaya, lakini michango hii ambayo tunaizungumzia hapa inaweza ikawa ni ile michango ambayo wazazi wenyewe kupitia mikutano ya wazazi na kamati za shule wanakubaliana, kwa mfano wanaweza wakasema wanataka wanafunzi wawe wanavipindi vya ziada, kwa hiyo wanakubaliana kutoa michango ya aina fulani, lakini michango mingine ni hii ambayo inafahamika ambayo ni michango ya uendeshaji wa shule ambayo kama nilivyojibu kwenye majibu ya msingi ukomo umewekwa kwa shule za bweni kidato cha tano ni shilingi 80,000 na kwa shule za kutwa ni shilingi 50,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye swali la pili la Mheshimiwa Mbunge, naomba niendelee kusisitiza maagizo ambayo yametolewa huko awali kwamba Maafisa Elimu wa Mikoa, wa Wilaya, wa Kata, Wakuu wa Shule hawaruhusiwi kukataa kuwapokea wanafunzi kwa sababu tu wamekosa pesa za michango.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba nisisitize hilo kwa sababu ni maelekezo ambayo tayari yalishatolewa, mwanafunzi asikataliwe kupokelewa shuleni kwa sababu amekosa pesa ya michango. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba nichukue nafasi hii kutoa wito kwa wazazi wa wanafunzi wa kidato cha tano wale waliyochaguliwa kuingia kidato cha tano waweze kuhakikisha kwamba wanawapeleka watoto wao shule hata kama hawajakamilisha michango au kuwa na sare, ni muhimu sana watoto wanapochaguliwa kwenda kidato cha tano waweze kwenda shuleni kuripoti. (Makofi)