Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Subira Khamis Mgalu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SUBIRA K. MGALU aliuliza:- Je, Serikali inachukua hatua gani kwa Maafisa Masuuli na Wahazini wa Serikali za Mitaa kutokana na ongezeko la hoja za ukaguzi za Ripoti za CAG?

Supplementary Question 1

MHE. SUBIRA K. MGALU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza, niipongeze sana Serikali yetu ya Awamu ya Sita kwa maboresho mbalimbali yaliyofanyika ambapo inaoneka kupitia Taarifa za CAG kuna mabadiliko makubwa katika usimamizi wa fedha za umma kutokana na kupungua kwa hati mbaya na hati za mashaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza. Kwa kuwa majibu yalitolewa na Serikali inaonesha hali ni nzuri na imezidi kuimarika hatua za kisheria zimechukuliwa, lakini kwa wananchi na umma bado dhana na tafsiri kwamba hali ya ubadhirifu na matumizi mabaya ya Serikali yameongezeka. Je, Serikali ipo tayari kuunda pengine kitengo kwa kushirikiana na Ofisi ya CAG na Ofisi pia ya Bunge kwenye Kamati zake ili kuelimisha umma wajue tafsiri sahihi na hatua zilizochukuliwa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kwa kuwa ukaguzi wa hesabu siyo suala la kuviziana, mkaguzi anapofika anafanya vikao, anapoondoka anafanya kikao, anaacha hoja na anatoa nafasi za siku 21 kujibiwa, lakini inatokea kwamba nafasi hiyo haitumiki vizuri na wakaguliwa (Maafisa Masuuli), kiasi kwamba hoja zote zinajitokeza kwenye Ofisi ya CAG kwenye ripoti yake, lakini baada ya kutoka ripoti hao hao wanatafuta majibu…

SPIKA: Mheshimiwa Subira, uliza swali, tafadhali.

MHE. SUBIRA K. MGALU: Mheshimiwa Spika, je, Serikali ipo tayari kufanya utafiti wa kujua tatizo ni nini ili iweze kuchukua hatua stahiki? Ahsante sana. (Makofi)

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Ni kweli, kama ambavyo jibu langu la msingi limesema hali ya ukaguzi kwa maana ya mwenendo wa hati katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa imeendelea kuimarika siku hadi siku kwa sababu ya hatua madhubuti ambazo zimechukuliwa na Serikali.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba bado kuna baadhi ya maeneo ambayo kuna matumizi yasiyostahili ya fedha za umma. Kwa hivyo, Serikali kama ambavyo nimetangulia kusema itaendelea kuchukua hatua na kuboresha mifumo ili kudhibiti matumizi mabaya ya fedha ya umma.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la Mheshimiwa Mbunge kwamba kianzishwe kitengo maalum kwa ajili ya kutoa elimu kwa umma. Tunapokea mawazo hayo ni mazuri, lakini halmashauri zetu zinaendelea kuelimisha wananchi kwamba Serikali inachukua hatua katika eneo hili.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la hati za ukaguzi kwamba kuna utaratibu wa mkaguzi kufanya exit meetings, lakini bado kunakuwa na hoja. Suala hili tumeendelea kulifanyia kazi kumekuwa na changamoto ya utunzaji wa document katika halmashauri zetu ambazo mara nyingine wakati wa ukaguzi hazipatikani mara moja lakini zinapatikana baada ya muda fulani.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tumeelekeza sasa halmashauri zetu zote wahakikishe document zote zinapatikana kwa wakati, wakati wakaguzi wa CAG wapo ili hoja zote zifungwe haraka iwezekanavyo badala ya kusubiri muda mrefu, ahsante.