Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Boniphace Nyangindu Butondo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kishapu

Primary Question

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO Aliuliza: - Je, lini usambazaji wa maji ya Ziwa Victoria katika Kata za Mondo, Busangwa, Sekebugolo na Mwasubi - Kishapu utakamilika?

Supplementary Question 1

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana, kwanza, ninaomba niipongeze Serikali kwa kazi kubwa inayofanya ya usambazaji wa maji katika Wilaya yangu na Jimbo langu la Kishapu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi ninapongeza usanifu wa kina uliofanyika ambao una thamani ya jumla ya shilingi bilioni 16.5 ambayo kimsingi itakwenda kutatua tatizo la maji katika kata hizi tatu.

Swali, je, Serikali iko tayari sasa kwa mwaka wa fedha 2025/2026 kuhakikisha kwamba inatekeleza miradi hii? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ninaiomba Serikali iweze kunihakikishia kama itaweza kufanya usanifu wa kina katika Kata ya Masanga, Kata ya Mwamalasa pamoja na Kata ya Kiloleli. Hizi ni kata ambazo zina changamoto kubwa ya maji na bahati zuri yako matoleo ya Mradi wa Maji ya Ziwa Victoria. Je, Serikali iko tayari kufanya upembuzi wa kina ili mradi sehemu hii na yenyewe iweze kupata huduma ya maji? (Makofi)

Name

Kundo Andrea Mathew

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bariadi

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana na pia ninamshukuru sana kaka yangu Mheshimiwa Boniphace Nyangindu Butondo, Mbunge wa Kishapu. Ninampongeza sana kwa kazi kubwa ambayo ameendelea kuifanya kwa Wana-Kishapu. Hakika Wanakishapu wamepata mwakilishi mahiri kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata usanifu huu uliofanyika wa kuhakikisha kwamba tunaangalia huduma ya upatikanaji wa maji na tukaja na hii figure ya shilingi bilioni 16.1, ni kwa sababu ya umahiri wa Mheshimiwa Butondo kwa kushirikiana na Serikali ya Chama cha Mapinduzi, lakini vilevile katika bajeti ya mwaka 2024/2025 tulitenga shilingi bilioni 3.4 kwa ajili ya miradi ndani ya Kishapu, lakini katika bajeti hii pia Mheshimiwa Butondo tumemuongezea kwa ajili ya wananchi wake wa Kishapu shilingi bilioni 1.77, kwa ajili ya kuhakikisha kwamba miradi mingine inaendelea kutekelezwa, lakini nimtoe hofu, Serikali iko tayari kutenga fedha hizi katika bajeti ijayo ili kuhakikisha kwamba sasa tunaenda kutekeleza mradi huo kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge ameomba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Kata za Kiloleni, Masanga pamoja na Mwamalasa. Mheshimiwa Mbunge nikutoe hofu, wewe mwenyewe umesema kwamba kuna Mradi wa Ziwa Vikroria kazi iliyobaki pale ni kufanya usanifu na Serikali tuko tayari kwenda kufanya usanifu, lengo ni kwamba wananchi wako wapate huduma ya majisafi na salama kutoka Ziwa Viktoria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana.

Name

Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Primary Question

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO Aliuliza: - Je, lini usambazaji wa maji ya Ziwa Victoria katika Kata za Mondo, Busangwa, Sekebugolo na Mwasubi - Kishapu utakamilika?

Supplementary Question 2

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi wa Maji Mogitu Gehandu, awamu ya kwanza imekamilika na awamu ya pili ambako sehemu kubwa ya Kata ya Gehandu imepata maji. Lini awamu ya tatu itakamilika ili maji yaweze kufika Gidabwanja, Marega, Mwanina, Milongori na eneo la Alosabida?

Name

Kundo Andrea Mathew

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bariadi

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana kaka yangu mhandisi kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya na nimuombee kwamba mambo yake yaende vizuri, lakini kwenye mradi wa awamu ya kwanza ni kazi yake kubwa, awamu ya pili ni kazi yake kubwa ambayo ameifanya kwa kushirikiana na Serikali ya Chama Cha Mapinduzi katika utekelezaji wa Ilani ya CCM, lakini vilevile nimuahidi, huu mradi wa awamu ya tatu, sisi ni kipaumbele cha Serikali kutokana na maombi yako kwa ajili ya wananchi wako. Nikutoe hofu katika bajeti hii inayokuja tunaenda kuhakikisha kwamba mradi huo unatekelezwa kwa awamu ya tatu ilimradi wananchi wa eneo lako wapate huduma ya majisafi na salama, ahsante sana.

Name

Vincent Paul Mbogo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkasi Kusini

Primary Question

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO Aliuliza: - Je, lini usambazaji wa maji ya Ziwa Victoria katika Kata za Mondo, Busangwa, Sekebugolo na Mwasubi - Kishapu utakamilika?

Supplementary Question 3

MHE. VINCENT P. MBOGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi, nina swali dogo moja la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kijiji cha Ntemba, Kata ya Kate hakina maji kabisa, lini Serikali mtapeleka maji katika Kijiji cha Ntemba na kuwasambazia wananchi?

Name

Kundo Andrea Mathew

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bariadi

Answer


NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kujibu swali la nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti yetu ambayo Mheshimiwa Waziri wa Maji Jumaa Hamidu Aweso jana aliiweka mbele ya Bunge lako Tukufu, imeangalia sana Jimbo la Nkasi ambako Mheshimiwa Mbunge anatoka na ni lengo la Serikali kutokana na Ibara ya 100 ya Ilani ya Chama Cha Mapinduzi, Serikali itahakikisha kwamba inafikisha miradi ya maji vijijini ili kuhakikisha kwamba tunaendelea kuenzi na kuhakikisha kwamba ajenda ya kumtua mama ndoo kichwani iliyoasisiwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, inaonekana kwa vitendo. Lengo ni kwamba ionekane pale ambako watu wanachota maji katika maeneo ya makazi bila kuwa na changamoto yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mbunge tutafanyia kazi kwa umakini mkubwa sana, ahsante sana. (Makofi)

Name

Cecil David Mwambe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ndanda

Primary Question

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO Aliuliza: - Je, lini usambazaji wa maji ya Ziwa Victoria katika Kata za Mondo, Busangwa, Sekebugolo na Mwasubi - Kishapu utakamilika?

Supplementary Question 4

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa na mimi nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao mradi wa maji ambao Serikali ilitenga zaidi ya shilingi milioni 950 kwenye hii Kata ya Ndanda mpaka utakapokuwa umekamilika, lakini mradi huu unapokwenda kuhudumia Vijiji vya Liputu, Tuungane, Mpoora; Njinga pamoja na Majengo.

Swali, wakati wa usanifu wa mradi huu, walikuwa hawajatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa chujio na wananchi wa kata hiyo kwa kipindi fulani hasa wakati mvua zinanyesha wanapata maji machafu.

Je, Serikali haioni haja ya kutenga pesa kwa ajili ya kujenga chujio ili kuwaondolea adha wakazi wa Ndanda waweze kupata majisafi, salama na ya kutosha? (Makofi)

Name

Kundo Andrea Mathew

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bariadi

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana na nimshukuru sana kaka yangu Mheshimiwa Cecil Mwambe, ni ushauri mzuri sana kwa Serikali, na lengo la Serikali ni kwamba wananchi wapate majisafi na salama na kama wananchi wanapata maji ambayo hayaridhishi na solution kama ni kuweka chujio, Serikali haitochelewa kuchukua hatua stahiki kuhakikisha kwamba tunaenda kujenga chujio ili wananchi wapate huduma ya maji yaliyo safi, salama na toshelevu na yenye bei ambayo inakubalika, ahsante sana.

Name

Kunti Yusuph Majala

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO Aliuliza: - Je, lini usambazaji wa maji ya Ziwa Victoria katika Kata za Mondo, Busangwa, Sekebugolo na Mwasubi - Kishapu utakamilika?

Supplementary Question 5

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru, Mradi wa Maji Wilaya ya Chemba, Kelema Maziwani pamoja na Ovada, vifaa tunavyo, lakini pili miundombinu yote imekamilika na mabomba tunayo, tunahitaji shilingi milioni 214 ili tukamilishe usambazaji wa maji kwa wananchi wetu. Je, ni lini mtatupatia fedha hizi ili wananchi wetu waweze kupata huduma hii bora ya maji?

Name

Kundo Andrea Mathew

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bariadi

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana na nimshukuru sana dada yangu Mheshimiwa Kunti kwa kuwasemea Wananchi wa Kata ambazo amezitaja, lakini pia kwanza ametambua Serikali tayari imeshafanya hatua ya kwanza, mradi umeshaanza tayari bomba zimeshakuwepo pale, maana yake ni kwamba zaidi ya 70% imeshafanyika. Kwa hiyo 30% kama ambavyo anaomba hizi fedha shilingi milioni 200, Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan haiwezi kushindwa kutoa shilingi milioni 200 ili kukamilisha mradi huo na wananchi wake wapate huduma ya majisafi na salama. Mheshimiwa Mbunge ninakuahidi hilo tunalichukua na tunaenda kulifanyia kazi kwa uzito stahiki, ahsante sana.