Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Khatib Said Haji

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Konde

Primary Question

MHE. KHATIB SAID HAJI aliuliza:- Kuchelewesha haki ni kunyima haki. Je, Jeshi la Polisi limejitathmini juu ya utendaji wake, hususan katika Idara ya Upelelezi wa Makosa mbalimbali kabla ya kuyafikisha mashtaka mahakamani?

Supplementary Question 1

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ufanisi na utendaji wa Mahakama unategemea ushahidi katika utendaji wake, lakini imekuwa ni jambo la kawaida ukiwa katika Mahakama zetu mara baada ya kusomwa Shauri Namba, Waendesha Mashtaka kusimama na kuiambia Mahakama tunaomba Mheshimiwa Hakimu au Jaji uahirishe shitaka hili kwa sababu upelelezi haujakamilika, hivyo ni vitu vya kawaida sana.
Je, Serikali kwa kushindwa kupeleka ushahidi haraka katika Mahakama kwa kesi zinazoendelea ndiyo chimbuko la kusababisha mlundikano wa mahabusu katika Magereza yetu na jambo hilo ndilo linalosababisha wananchi wengi kukosa imani na Mahakama na kuona hazitendi haki, je, hamuoni kwamba kuchelewesha kupeleka ushahidi katika Mahakama mnasababisha lawama kwa Mahakama ambazo kimsingi siyo za kwao? (Makofi)
Swali la pili, katika nchi yetu lilitokea tukio kubwa na baya la ugaidi ambalo lilisababisha maisha ya watu wetu kupotea katika Ubalozi wa Marekani pale Dar es Salaam. Kuna watuhumiwa ambao walichukuliwa hapa kwenye nchi yetu na wakapelekwa Marekani kwa ajili ya mashtaka hayo na upelelezi wa makosa hayo, lakini haikuchukua zaidi ya miaka miwili watuhumiwa wale walionekana hawakuwa na makosa na wakaachiwa huru Marekani na Tanzania.
Je, ni kwa nini mpaka leo watuhumiwa wa ugaidi, Mashekhe wa Uamsho kutoka Zanzibar ambao hawakuua hata kuku katika mashtaka yao, mpaka leo mmeendelea kuwashikilia ilihali mmeshindwa kupeleka ushahidi. Mpaka lini Serikali mtaendelea kuwashikilia wazee wa watu wale na mmeshindwa kuthibitisha makosa yao? (Makofi)

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI:
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la upelelezi ni jambo la msingi ili kuhakikisha kwamba haki inatendeka. Lazima Jeshi la Polisi lifanye uchunguzi wa kina na kujiridhisha juu ya makosa ambayo yamefanywa na mtuhumiwa ili hatimae mtuhumiwa yule aweze kutendewa haki. Kwa hiyo, ninaomba Mheshimiwa Mbunge aelewe kwamba siyo dhamira ya Serikali wala Jeshi la Polisi kuchelewesha upelelezi, lakini kuna aina ya makosa ambayo yanahitaji kufanyiwa kazi ya ziada ambayo yanahusisha taasisi nyingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano kunahitaji kufanyika utafiti kutoka katika vyombo na mamlaka nyingine, masuala ya mawasiliano kwa mfano TCRA, kuna masuala yanayohusu uhamiaji, masuala ya taasisi nyingine mbalimbali za ndani na nje ya nchi. Kwa hiyo, ili kuweza kuhakikisha kwamba mtuhumiwa yule anatendewa haki lazima Jeshi la Polisi lipate muda wa kutosha. Hakuna Serikali ama chombo chochote cha Serikali kinachohitaji kumkomoa mwananchi wake, hilo la kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili kuhusiana na suala la watuhumiwa wa Uamsho. Tuhuma ambazo zinawakabili watu hawa ni nzito, kwa hiyo basi ni lazima uchunguzi wa kina vilevile ufanyike ambao utahitaji muda. Kwa hiyo, naomba jambo hili kwa kuwa liko Mahakamani siyo busara kwa mujibu wa sheria za nchi na Katiba ya nchi hii kulijadili katika Bunge hili Tukufu, tuacha mamlaka husika na mhimili wa dola ufanye kazi yake.