Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Saed Ahmed Kubenea

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Ubungo

Primary Question

MHE. SAED A. KUBENEA aliuliza:- Kumekuwepo na vitendo vingi vya uhalifu hapa nchini kwa watu kuvamiwa, kupigwa, kujeruhiwa na kuporwa mali zao na hata kuuawa:- • Je, Serikali ina mpango gani wa kukomesha vitendo hivyo vya uhalifu ambavyo vinatishia usalama wa raia na mali zao? • Je, Serikali haioni umuhimu wa kuongeza juhudi za ulinzi wa raia na mali zao ili kudumisha amani na utulivu nchini?

Supplementary Question 1

MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Pamoja na majibu ya Naibu Waziri, swali langu msingi wake ni kwamba, wananchi ambao wameumizwa, wametekwa, wamepotea, sio suala la kuimarisha Vituo vya Polisi kwenye ulinzi shirikishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu je, Serikali ina mpango gani wa kushikika wa kulinda raia hawa ambao wamekuwa wakijitolea kutetea nchi yao kwa maslahi ya Watanzania wote?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni lini Serikali itakamilisha uchunguzi na kuleta ripoti Bungeni ya matukio ya kihalifu yanayofanana na ugaidi ambayo wamefanyiwa watu mbalimbali, akiwemo Mheshimiwa Tundu Lissu, Mwandishi wa Habari wa Gazeti la Mwananchi, Abisalom Kibanda na Dokta Stephen Ulimboka na wengineo? (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nataka nichukue fursa hii kumpinga na kumkosoa vikali kabisa Mheshimiwa Saed Kubenea, kutokana na utangulizi wa swali lake ambalo ameuliza; na kimsingi Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kupitia Jeshi la Polisi, imekuwa ikihakikisha inalinda usalama wa raia wote na mali zao. Hakuna matabaka katika kusimamia ulinzi wa raia na mali zao, hiyo ndio kazi ya Jeshi la Polisi ya kila siku kwa hiyo, kusema kwamba kuna watu wanakosoa Serikali, sijui kuna watu wana nini, hizo ni kauli potofu na si sahihi na nadhani kwa mamlaka yako ungeelekeza hata zifutwe katika Hansard. Kwa sababu, ni upotoshwaji mkubwa kwa jamii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika hilo suala la kulinda usalama wa raia na mali zao jitihada kubwa zimekuwa zikifanyika. Imani yangu ni kuwa kwa kadri ambavyo tunakwenda mbele tumekuwa tukifanya hivyo kwa kutumia mbinu mbalimbali za kitaalam, kukusanya taarifa za kiintelijensia, kufanya doria, kuangalia maeneo tete, kuangalia takwimu, kumbukumbu za uhalifu nchini na ndio maana mpaka leo nchi yetu imeendelea kuwa salama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoelekea katika Serikali ya Uchumi wa Viwanda, Serikali ya Uchumi wa Kati, tunaamini kabisa kutakuwa kuna mabadiliko makubwa sana ya kiteknolojia katika utekelezaji wa majukumu yake kwenye vyombo vyetu vya dola. Kwa hiyo, tutakapoimarisha na kuwekeza katika maeneo ya teknolojia tunaamini kabisa kazi hii itafanywa katika mazingira mepesi zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusu uchunguzi. Kazi ya uchunguzi imekuwa ikiendelea kufanyika, ingawa kazi ya uchunguzi kama alivyozungumzia yeye katika eneo mahususi la ugaidi, lina changamoto nyingi kwa sababu, tuhuma za ugaidi zinahusisha taarifa nyingine ambazo zinatoka katika mamlaka za nchi nyingine, lakini na taasisi nyingine nje ya Jeshi la Polisi. Kwa hiyo, katika kufanya uchunguzi ambao unahitaji taarifa kupata katika nchi nyingine, kupata katika mamlaka nyingine, si jambo ambalo linaweza likawa limefanyika kwa wakati mmoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, mpaka sasa kutokana na matukio mengi yaliyojitokeza kuna hatua kubwa imeshafikiwa katika uchunguzi wa kesi mbalimbali, ziko ambazo zimeshafika mwisho, ziko ambazo zinaendelea kuchunguzwa. Pale ambapo uchunguzi utakamilika hatua zitachukuliwa kwa wahusika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe wito kwa watu wote ambao wanahusika kutoa ushirikiano kwa mamlaka katika kutekeleza majukumu yake. Mfano huu ambao ameuzungumzia wa kesi ya Mheshimiwa Tundu Lissu, tumekuwa mara nyingi tukitaka ushirikiano kutoka katika chama hiki ambacho Mheshimiwa Kubenea anatoka, ili tuweze kupata watu ambao wanaweza kutusaidia kutupa taarifa, ikiwemo dereva yule ambaye alikuwa na Mheshimiwa Tundu Lissu, lakini wenyewe wamekuwa wakifanya jitihada za kufifisha kupatikana kwa dereva huyo. Kwa hiyo, ushirikiano kwa wananchi ikiwemo na wewe mwenyewe Mheshimiwa Mbunge na chama chake ni muhimu katika kukabiliana na kuharakisha uchunguzi wa kesi yetu. (Makofi)