Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Ezekiel Magolyo Maige

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Msalala

Primary Question

MHE. EZEKIEL M. MAIGE (K.n.y. MHE. AHMED A. SALUM) aliuliza:- Waziri Mkuu alipofanya ziara katika Mkoa wa Shinyanga aliahidi ujenzi wa Vituo viwili vya Afya katika Jimbo la Solwa:- Je, ni lini ahadi hiyo itatekelezwa?

Supplementary Question 1

MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kuniona na kunipa nafasi, lakini pia naomba nimshukuru sana Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri. Pamoja na majibu hayo, naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza.

Swali la kwanza; Mheshimiwa Waziri Mkuu pia alifanya ziara katika Halmashauri ya Wilaya ya Msalala na kwa kuona hali ilivyokuwa na hasa wananchi walivyojitolea kuunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Tano katika kukabiliana tatizo la afya, alikubali pia kutushika mkono kwa kutupatia shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya cha Isaka. Nataka kufahamu ni hatua gani imefikiwa katika utekelezaji wa ahadi hiyo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu?

Swali la pili; kama ambavyo Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba kuna Halmashauri 67 ambazo zimepatiwa shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi kwa Hospitali za Wilaya, kwa bahati mbaya Halmashauri ya Wilaya ya Msalala haina hospitali ya Wilaya na haiko katika hizi Halmashauri 67. Nataka kufahamu: Je, itawezekana sasa kwa awamu hii ambayo itakuwa ni ya pili mwaka 2019/2020 Halmashauri hii nayo ikatengewa hiyo fedha ili na yenyewe iweze kupata Hospitali ya Wilaya?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, kipekee kwanza naomba nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Maige na wananchi wake jinsi ambavyo wamekuwa wakijitolea katika suala zima la afya, wamejenga maboma mengi kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na swali lake wakati Mheshimiwa Waziri Mkuu ametembelea Msalala na akahaidi kwamba na Kituo cha Afya Isaka nacho kingeweza kupatiwa fedha; ni ukweli usiopingika kwamba Isaka ni miongoni mwa eneo ambalo lina watu wengi na iko haja ya kuhakikisha kwamba kunakuwa na Kituo cha Afya ili kupunguza adha ya wananchi wengi kupata huduma ya afya. Naomba aendelee kuiamini Serikali kama ambavyo nimejibu katika swali langu la msingi kwamba kwa kadri fursa ya fedha inapopatikana ni wajibu wetu kuhakikisha kwamba ahadi zote za viongozi wa Kitaifa tunazitekeleza. Nasi bado tunakumbuka hiyo ahadi, naomba Mheshimiwa Maige avute subira.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili ni kwamba katika Halmashauri 67, Halmashauri yake haikuwa miongoni mwa zile ambazo zilipata fursa ya kujengewa hospitali. Sina uhakika katika orodha ya hivi sasa hivi tuna jumla ya Halmashauri 27 ambazo katika bajeti, tutakapokuja kuomba fedha tutaenda kuongeza fedha katika Halmashauri nyingine 27. Tuombe Mungu katika hizo 27 na yake iwe miongoni mwake.

Mheshimiwa Spika, nashukuru.