Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Primary Question

MHE. QAMBALO W. QULWI aliuliza:- Kijiji cha Makhoromba ni kati ya vijiji 10 vilivyopangwa kunufaika katika mpango wa WSDP-I Wilayani Karatu. Hadi hivi sasa Wilayani Karatu mradi wa maji katika kijiji hicho haujatekelezwa:- Je, ni lini Serikali itatekeleza mradi huo ili wananchi hao waondokane na tatizo kubwa la kukosa huduma ya maji?

Supplementary Question 1

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Hali ya upatikanaji wa maji katika kijiji hicho ni mbaya sana, ukiongea habari ya vituo vitatu kwa wananchi zaidi 5,000 ni chini kabisa ya kiwango ambacho kinaruhusiwa. Sasa nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, Mheshimiwa Waziri anajua Halmashauri ya Wilaya ya Karatu ina idadi ndogo ya watumishi katika sekta ya maji na kazi za kitaalam alizozielekeza kwa idadi ya wataalam tulionao haitaweza kukamilika. Je, yuko tayari sasa kuongeza nguvu ya uhandisi na wataalam wa survey ili kazi hiyo aliyoelekeza ifanyike kwa muda unaotakiwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, vyombo vya watumia maji, mfano, Bodi za Maji, Mamlaka Jumuiya za Watumia Maji na Kamati za Maji zinatambulika kisheria na vimetoa huduma za usimamizi na uendelezaji wa miradi ya maji. Hivi karibuni Serikali imesimamisha uchaguzi wa chombo cha maji kinachoitwa KAVIWASU pale Karatu ambacho kimetoa huduma hiyo kwa zaidi ya miaka 20. Je, ni halali Serikali kuingilia mchakato wa kupata viongozi wa wananchi ili waweze kusimamia chombo chao? Ahsante.

Name

Jumaa Hamidu Aweso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Pangani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake zuri, lakini kubwa sisi kama Wizara ya Maji tunatambua changamoto kubwa sana ya maji Karatu na ndio maana tuna mradi mkubwa sana wa TOM zaidi ya milioni 650 ambao tunautekeleza. Kikubwa tunatambua utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na watumishi wa kutosha wenye weledi na wenye uwezo na sisi kama Wizara ya Maji ndio maana tukaja na Wakala wa Maji. Nataka nimhakikishie uanzishwaji wa wakala ule tutahakikisha tunaweka wataalam wetu wa kutosha na katika eneo lake ili mwisho wa siku wananchi wa Karatu waweze kupata maji safi, salama na yenye kutosheleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu chombo cha watumiaji maji, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge hilo nimelipokea hebu tulifuatilie kwa ukaribu ili tuweze kulitolea ufafanuzi wa haraka. Ahsante sana.