Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Maryam Salum Msabaha

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:- Kumekuwa na matukio ya mara kwa mara ya watoto wachanga kutupwa majalalani, mitaroni na katika mifuko ya rambo:- (a) Je, nini kauli ya Serikali kuhusu matukio hayo? (b) Je, ni watuhumiwa wangapi walishakamatwa na kuchukuliwa hatua za kisheria?

Supplementary Question 1

MHE. MARYAM SALUM MSABAHA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, katika tafiti nilizozifanya kuna makundi manne, kuna kundi la hawa watoto wanaofanya kazi majumbani, akina mama ambao wanajiuza na wanafunzi. Swali linakuja hivi, kuna akina baba ambao wana akili zao timamu na wengine ni watu wa Serikali wamekuwa wakiyalaghai makundi haya niliyoyataja na kuwapa ujauzito na wakati wanawafuata labda wanataka huduma za kijamii wanawatosa na wengine kuwatishia na bunduki. Naomba kujua ni nini kauli ya Serikali kwa wale wanaobainika kuhusika na matukio haya? Watu hawa wanapopelekwa kwenye Vituo vya Polisi au Serikali za Mitaa wachukuliwe hatua za kinidhamu na sheria kali ili iwe fundisho kwa wengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa majiji makubwa Mwanza, Arusha, Dodoma, Dar es Salaam na Mbeya, yamekuwa na ongezeko la wanawake ambao wanafanya biashara za kujiuza (biashara za ngono). Je, Serikali ina mikakati gani hasa katika Jiji la Dodoma ambalo ni Makao Makuu ya Serikali kudhibiti hali hii ili kupunguza ongezeko la kutupa watoto majalalani? Naomba kauli ya Serikali. (Makofi)

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, hakuna kitu chochote ambacho kinaweza kuhalalisha juu ya hatua yoyote ambayo atachukua mama kumtupa mtoto wake. Pili, wale ambao wanahusika kuwapa ujauzito mabinti hawa wadogo ambapo wengine ni wanafunzi na wale ambao amewataja, imeelezwa wazi katika sheria kama ambavyo nimejibu katika swali langu la msingi kwamba kuna Sheria ya Mtoto lakini pia Kanuni ya Adhabu ambazo zinaelezea wajibu wa mtu ambaye ameamua kuzaa mtoto kwa hiari yake ama amejitolea kuwa mlezi wa mtoto yule na jinsi ambavyo sheria inazungumza kwa wale ambao watashindwa kutekeleza wajibu huo. Kwa hiyo, sheria iko wazi na adhabu inaeleza kwamba kwa mtu ambaye atashindwa kuhudumia mtoto wake kutimiza wajibu huo anaweza kufungwa kifungo kisichopungua miaka mitano. Kwa hiyo, sheria iko wazi katika eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na hoja yake ya pili kuhusu madada wanaojiuza, sina hakika kama utafiti wake aliouzungumza una usahihi kiasi gani kuhusu mahusiano ya akina mama ambao wanatupa watoto na wale madada wanaojiuza. Hata hivyo, niseme tu kwamba Jeshi la Polisi limekuwa likifanya jitihada mbalimbali kukabiliana na aina ya watu ambao wanafanya biashara haramu ikiwemo biashara za ngono.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe wito kwa wananchi wote kwa ujumla ikiwemo na akina baba kujiepusha kuwa wateja wa biashara hizo. Kwa hiyo, hapa ni shilingi inaangaliwa pande zote mbili, kwa hawa akina dada ambao wanafanya biashara hizi lakini mpaka wanunuzi wa biashara hizi. Kwa hiyo, wote wawili wanafanya makosa na pale ambapo watabainika basi sheria itachukua mkondo wake.