Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Primary Question

MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza: - Je, ni lini majengo yataongezwa katika Chuo cha VETA Urambo ili kuongeza fani ambazo hazitolewi kwa sasa?

Supplementary Question 1

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa mwenyekiti ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa niaba ya Serikali alivyojibu; amejibu vizuri, ahsante.

Swali la kwanza; tuna uhaba wa walimu sita na katibu muhitasi mmoja na uhaba huu unasababisha kwamba mwalimu wa fani moja anapokuwa hayupo hakuna linaloendelea;

Je, Serikali ina mpango gani wa kutuongezea wafanyakazi saba ili shughuli za utoaji wa elimu ya ufundi ziendelee kama zilivyopangwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili jambo muhimu katika mafunzo ya ufundi ni utendaji, yaani practical sasa utendaji au elimu kwa vitendo unahitaji sana vifaa;

Je, Serikali yetu imejipangaje kuhusu upatikanaji wa vifaa ili kweli mafunzo ya ufundi ya vitendo yafanyike?

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Margaret Sitta, Mbunge wa Urambo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimuondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge, Serikali ya Awamu ya Sita imejidhatiti kuhakikisha kwamba vyuo hivi ambavyo vilikuwa havina miundombinu tunaenda kuongezea miundombinu. Na hatukufanya hivi tu kwa chuo hiki cha Urambo peke yake, kuna vyuo kadhaa ambavyo vilikuwa na upungufu wa miundombinu. Tunafahamu upungufu wa miundombinu kwa Mheshimiwa Mwijage kule Muleba, tumeshafanya kazi kule, Mheshimiwa Rais alitoa fedha kwa ajili ya ukarabati pamoja na ujenzi wa miundombinu mingine. Pia kwa Mheshimiwa Dugange kule Wanging’ombe tumefanya hivyo; kwa Mheshimiwa Mtanda Serikali imepeleka fedha vilevile lakini vilevile tumepeleka fedha kule Mikumi kwa Mheshimiwa Londo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, si hicho tu, katika swali lake la kwanza anataka kufahamu mkakati wa Serikali juu ya walimu. Nimuondoe wasiwasi, Mheshimiwa Rais alitoa kibali cha kuajiri wafanyakazi watumishi wakiwemo na hao walimu 571. Mpaka hivi sasa ninavyozungumza walimu 151 tayari wameshaajiriwa na wameshapelekwa kwenye maeneo mbalimbali ikiwemo na kwenye baadhi ya hivi vyuo ambavyo vilikuwa tayari vinatoa huduma na vile vyuo vytu 25 vya wilaya na vinne vya mikoa. Kwa hiyo tunaendelea na mchakato huu kwa kukamilisha idadi hii ya waaalimu na watumishi 571 tunaamini na Urambo itafikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa vifaa naomba nimtoe wasiwasi Mheshimiwa na Bunge lako tukufu, tumejidhatiti na kujipanga kwa dhati kabisa kuhakikisha kwamba tunapeleka vifaa kwenye vyuo hhivi vile vya zamani lakini na vile vipya ambavyo tunajenga hivi sasa. Katika bajeti yetu hii inayoendelea tuna package ya vifaa lakini vilevile na katika bajeti ambayo tumeanza kuisoma hapa kutakuwa na eneo la fedha ambayo tumetenga kwa ajili ya ununuzi wa vifaa kwa ajili ya vyuo hivi vya VETA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.