Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Dr. Oscar Ishengoma Kikoyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muleba kusini

Primary Question

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO aliuliza:- Je, ni maprofesa wangapi wanaozalishwa kila mwaka na ni wangapi wanastaafu kwa kipindi hicho?

Supplementary Question 1

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa majibu ya Serikali ni majibu mazuri lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia idadi ya Maprofesa nchini imeporomoka sana kwa kipindi cha miaka 10 iliyopita. Chuo Kikuu pekee cha Dar es Salaam kinahitaji Maprofesa 161 lakini wapo Maprofesa tisa. Sasa kwa nini Serikali isibadili umri wa kustaafu kutoka miaka 65 mpaka miaka 70 ili kutunza hao wachache tulionao? (Makofi)

Swali la pili, kwa nini Serikali sasa kwa kuwa tunao uhitaji mkubwa wa Maprofesa isitoe package nzuri ili kuwavutia vijana wengi wakajitahidi kufanya research ili waweze kufikia hiyo hatua ya Uprofesa kwa ajili ya kutunza vyuo vyetu vikuu?

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Kikoyo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi, Serikali imeendelea kuchukua hatua za kukabiliana na upungufu wa watumishi na taaluma katika vyuo vyetu vikuu vya umma nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kufanya mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza, tunaendelea kuongeza nafasi za ajira kwa Wahadhiri pamoja na Wanataaluma katika vyuo vyetu. Jambo la pili, tunaendelea kuruhusu uhamisho wa watumishi wenye sifa kutoka taasisi nyingine za Serikali ili kuweza kuingia katika Vyuo Vikuu na kuhudumu kama Wahadhiri pamoja na kwenda kwenye nafasi za juu za Uprofesa. Jambo la tatu, tunaendelea kusomesha Wahadhiri ndani na nje ya nchi ikiwa na lengo pana la kuhakikisha tunaongeza idadi ya watumishi au wanataaluma hawa katika vyuo vikuu. naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, Serikali itaendelea kufanya mambo haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile katika mradi wetu wa HEET wa miaka mitano ambao tunaendeleanao. Serikali inaenda kusomesha Wanataaluma zaidi ya 600 ambapo tunaamini kabisa katika usomeshaji huu tutaweza kupata maprofesa wengi. Kwa hiyo, nimwondoe wasiwasi juhudi hizi zinaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika jambo hili la kuongeza umri kwa wanataaluma hawa hasa Maprofesa, uliongezwa kutoka miaka 60 mpaka miaka 65. Mheshimiwa Mbunge hapa anashauri kwamba tuongeza tena iwe miaka 70. Tunachukua ushauri huu, tutakwenda kuufanyia kazi tuweze kuangalia namna bora ya kufanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo la pili kuhusu kuongeza maslahi Serikali imekuwa ikifanya hivyo. Serikali hii ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea na jambo hili vizuri kabisa na imeendelea kuboresha maslahi ya watumishi wakiwemo na wenzetu wanataaluma katika vyuo vikuu na tutaendelea kufanya hivyo kwa kadri ya bajeti itakavyoruhusu, nakushukuru.