Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Maimuna Ahmad Pathan

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MAIMUNA A. PATHAN aliuliza:- Je, ni lini tatizo la kukatika umeme mara kwa mara Mkoani Lindi litakwisha?

Supplementary Question 1

MHE. MAIMUNA A. PATHAN: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda kuwapongeza viongozi wa TANESCO Mkoa wa Lindi na Kanda ya Kusini, kuna Mkurugenzi wa Kanda Eng. Makota, kuna Meneja wa Mkoa wa Lindi Eng. Kahinda na mameneja wa Wilaya zote Mkoa wa Lindi wamejitahidi sana kubadilisha hali ya umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Je, Serikali imejipangaje kuhakikisha Grid ya Taifa inapita katika Wilaya zote za Mkoa wa Lindi na Mtwara ili kuondoa adha hii ya umeme?

Swali la pili, gesi kwa asilimia kubwa inatoka Mkoa wa Lindi na Mtwara lakini wenyeji wa Mkoa wa Lindi na Mtwara mpaka sasa hivi wanatumia kuni na nishati ya mkaa kupikia. Je, Serikali haioni sasa ni wakati mwafaka wa kuwasaidia kuwapelekea umeme wananchi wale ili tuweze kulinda mazingira ya nchi yetu?

Name

Stephen Lujwahuka Byabato

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kwa niaba ya Wizara na Serikali kwa ujumla nipokee pongezi kwa ajili ya hawa watendaiji wa TANESCO ambao wanafanya kazi nzuri na wanajitahidi kuhakikisha kila eneo kwa kweli huduma ya umeme inakuwa ya kuimarika. Niwaahidi Waheshimiwa Wabunge kwamba sisi Serikalini na wizarani na wenzetu wa TANESCO tutaendelea kuhakikisha jambo hili tunalifanyia kazi kwa sababu ndio kazi yetu ambayo mmetuamini nayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo la pili kwa sababu Mkoa wa Lindi tayari unayo miundombinu ya umeme, tutakapokuwa tumefikisha Grid pale Masasi au Tunduru tayari Mikoa yote na Wilaya zote za Mkoa wa Lindi zitakuwa zimepata umeme wa Grid ya Taifa. Kitakachoendelea kufanyika ni kuendelea kusambaza umeme kwa kutumia miradi yetu ya REA kwenye vijiji na vitongoji ili kila mwananchi sasa aweze kupata umeme. Kwa hiyo, miradi hii mitatu mikubwa niliyoisema itakapokuwa imekamilika na Gridi itakuwa imeingia Mkoa wa Lindi na tayari kila wilaya itapata.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo la pili kama tunavyofahamu sote Serikali imeanza sasa jitihada kubwa sana za kuhakikisha wananchi wote wanatumia nishati safi ya kupikia ambayo ni pamoja na gesi asilia, gesi za viwandani lakini pia na umeme, na katika maeneo yote ya Lindi na Mtwara tutaweka nguvu za ziada na jitihada kuhakikisha, zile nyumba chache ambazo tayari zimeunganishwa na gesi ya asili basi zinaongezeka kutoka kwenye idadi iliyopo kwa miradi ambayo tumeipanga kwenye bajeti inayokuja ili wananchi wengi zaidi waweze kutumia gesi asilia na hii mitungi mingine ya kawaida ya kuweza kupata nishati safi ya kupikia.