Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Seif Khamis Said Gulamali

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manonga

Primary Question

MHE. SEIF K. S. GULAMALI aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kuunga mkono wananchi wa Jimbo la Manonga kwa kuwasaidia kujenga madarasa mawili katika kila shule?

Supplementary Question 1

MHE. SEIF K. S. GULAMALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, kwanza niishukuru Serikali kutupatia fedha kwa ajili ya ujenzi wa shule za sekondari.

Swali langu la nyongeza, Mheshimiwa Waziri majibu yako yamejumlisha fedha zote zilizopo ndani ya Wilaya ya Igunga, hivyo basi nilikuwa nataka kuomba kwa shule zetu shikizi kwa maana ya Shule za Kazima, Mwakipanga, Mwamakingi pamoja na Shule ya Msingi Shikizi Mwasung’o. Je, ni lini Serikali itatuunga mkono kutupatia fedha kwa shule hizi shikizi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika Shule ya Sekondari ya Mwisi pamoja na Shule ya Sekondari ya Choma tuna uhaba wa mabwalo la chakula. Je, ni lini Serikali itatupatia fedha kwa ajili ya mabwalo kwa watoto wanaotumia kidato cha tano na cha sita? Ahsante.

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu maswali madogo mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Seif Khamis Said Gulamali, Mbunge wa Jimbo la Manonga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Shule Shikizi ambazo amezianisha Mheshimiwa Mbunge lini tutapeleka fedha, nimuhakikishie tu kwamba zipo katika mipango yetu na bahati nzuri siku ya Jumatatu tumezindua mradi wa BOOST na mradi ule unagharimu karibu trilioni 1.1. Kwa hiyo, fedha zile zitakapokuwa zimekuja maana yake tutazipeleka katika shule zote nchini ikiwemo ambazo Mheshimiwa Mbunge ameziainisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika mradi huo katika Shule ya Sekondari Mwisi ambazo hazina mabweni ni sehemu ya mpango ambao sisi kama Serikali tutapeleka maana yake ni component nzima ni pamoja na mabweni. Ahsante sana.

Name

Dr. Christina Christopher Mnzava

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SEIF K. S. GULAMALI aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kuunga mkono wananchi wa Jimbo la Manonga kwa kuwasaidia kujenga madarasa mawili katika kila shule?

Supplementary Question 2

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi kuuliza swali dogo la nyongeza.

Kwa kuwa Kata ya Mwasubi iliyopo katika Tarafa ya Mondo, Wilaya ya Kishapu ni kata mpya na haina madarasa ya kutosha katika shule ya sekondari. Je, ni lini Serikali itajenga ili kuongeza madarasa katika shule hiyo? (Makofi)

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuondoe hofu Mheshimiwa Mbunge tutaongeza madarasa kwa kuwa moja ya mpango wa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni kuhakikisha shule zote tunazifikia kwa kuongeza madarasa na kuzikarabati. Ahsante sana.